Quantcast
Channel: MPEKUZI
Viewing all 45270 articles
Browse latest View live

Wabunge Wataka CUF Ifutiwe Usajili

0
0

MBUNGE wa Viti Maalum (CCM), Munira Mustafa Khatib, ameitaka serikali kukifutia usajili Chama cha Wananchi (CUF), kwa madai kuwa kimekuwa kikishiriki katika matukio ya kupigwa na kuharibu mali za wananchi visiwani Pemba.

Mbunge huyo alitoa kauli hiyo jana, alipokuwa akiuliza swali la nyongeza katika kipindi cha maswali na majibu bungeni.
 
“Kutokana na kuwapo matukio ya wananchi kupigwa hususan wanachama wa CCM, ni kwanini serikali isikifutie usajili chama cha CUF kwakuwa ndio chanzo cha matukio hayo visiwani pemba,”alihoji Mbunge huyo.
 
Katika swali la Msingi la Mbunge wa Chambani (CUF), Yusufu Salim Hussein, naye alihoji kama serikali inatambua tatizo la raia kupigwa na kuharibiwa mali zao kwa upande wa Zanzibar, ambalo limekuwa likiongezeka siku hadi siku na hatua gani zimechukuliwa.
 
Kutokana na masuala hayo, wabunge walionekana wakisimama kuuliza maswali ya nyongeza na Mbunge wa Viti Maalum (CCM), Tauhida Cassian Nyimbo, alihoji serikali inachukua hatua gani kwa viongozi wa CUF ambao wamekuwa wakitoa kauli za vitisho kupitia mitandao ya kijamii na kuwafanya wananchi visiwani humo kuwa na hofu hasa kipindi hichi cha kuelekea sikukuu ya Idd el Fitri.
 
Naye Mbunge wa Dimani (CCM), Hafidh Ali Tahir, alihoji ni kwa namna gani serikali itawashughulikia baadhi ya viongozi ambao wamekuwa na tabia ya kuvunja sheria na maagizo ya viongozi kuhusu mikutano ya hadhara.
 
Akijibu maswali hayo, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Hamad Yusuf Masauni, alisema serikali inatambua kwamba kila unapofika wakati wa Uchaguzi Mkuu hasa katika kisiwa cha Pemba, baadhi ya watu hujichukulia sheria mkononi kwa kuwapiga wengine na kuharibu mali zao.
 
Kutokana na hali hiyo, alisema serikali itaendelea kuongeza vikosi vya ulinzi na usalama katika maeneo yote tete na kuhakikisha utii wa sheria bila shuruti unazingatiwa.
 
“Pia serikali itaendelea kuwaelimisha wananchi madhara ya kujichukulia sheria mikononi dhidi ya wengine wasio na hatia,” alisema Masauni.
 
Alitoa wito kwa wananchi wote kuacha mihemko ya itikadi za kisiasa wakati na kabla ya uchaguzi kwani hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yao.
 
Kuhusu viongozi wanaokiuka maagizo ya serikali kuhusu mikutano ya kisiasa, Masauni alisisitiza mikutano hiyo haitakiwi kwa wakati huu hadi hapo polisi itakapoona inafaa na kuvitaka vyama vya siasa kutii maagizo ya serikali.
 
“Hakuna mtu ambaye yuko juu ya sharia. Wale watakaoleta ukorofi watachukuliwa hatua kali bila kujali kama ni kiongozi wa aina gani na mahali gani anatokea. Lazima sheria ichukue mkondo wake,” alisema.
 
Kuhusu suala la kukifuta CUF, Naibu Waziri huyo alisema jukumu hilo si la serikali bali limo mikononi mwa Msajili wa vyama vya siasa, ambaye anatakiwa kuliangalia kwa mujibu wa sheria na taratibu zilizopo.
 
Aidha, alisema nchi iko salama na serikali itaendelea kuhakikisha amani na utulivu vinakuwapo wakati wa sikukuu hiyo na kuwataka wananchi kupuuza kauli za uchochezi zinazotolewa na wanasiasa.
 
Baada ya kipindi hicho, Mbunge wa Mwibara, (CCM), Kangi Lugola, aliomba mwongozo kwa Naibu Spika akisema ni kwa nini serikali ipo bungeni; isitoe majibu kuhusiana na matukio yanayofanywa na CUF ambayo mbunge mwenzake amependekeza kifutiwe usajili na badala yake inatoa jukumu kwa msajili wa vyama vya siasa wakati ni sehemu ya serikali.
 
Kutokana na mwongozo huo, Naibu Spika wa Bunge, Dk. Tulia Ackson, alisema atatoa majibu ya mwongozo huo baada ya kupitia sheria ya vyama vya siasa inasemaje.

Ufisadi wa kutisha watikisa vigogo 12 serikali ya Zanzibar

0
0
WATENDAJI 12 wa serikali ya Zanzibar, akiwamo Naibu Mhasibu Mkuu wa Serikali wamesimamishwa kazi kutokana na upotevu mkubwa wa fedha.

Akizungumza na waandishi wa habari visiwani Zanzibar jana, Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Khalid Salum Mohamed, alisema kati ya watendaji hao wamo wahasibu wakuu wa wizara sita wanaohusika na upotevu huo wa fedha.
 
“Kwa masikitiko makubwa naomba kutoa taarifa kuwa tumebaini upotevu wa fedha za serikali ambao tumeanza kuuchukulia hatua,” alisema waziri huyo.
 
Alisema upotevu huo wa fedha unaonekana sio wa bahati mbaya, bali ni jambo la kupangwa na umetekelezwa kwa njama za watendaji wa vitengo vya fedha uliowahusisha wahasibu.
 
Aidha, alisema hadi sasa kuna hundi zenye thamani ya Sh. milioni 571 zimeshindwa kulipwa kwa sababu ya uhalifu huo na hatua za awali za kutathmini upotevu huo zinaonyesha kuwa kiasi ambacho kinahusika na wizi huo kinaweza kuwa kikubwa zaidi ya hicho.
 
“Tulipopata taarifa za awali juu ya upotevu huu hatua za haraka zilichukuliwa na kubaini wahusika wakuu”alisema Dk. Khalid.
 
Alisema taarifa za awali zinaonyesha upotevu huo wa fedha umetokana na njama za baadhi ya watendaji wa kitengo cha malipo katika Wizara ya Fedha na Mipango wakishirikiana na baadhi ya wahasibu wa wizara tofauti za serikali.
 
Waziri huyo alisema hatua hiyo imezingatia matakwa ya Sheria ya Fedha za Umma namba 12 ya mwaka 2005 na kanuni zake na Sheria ya Utumishi wa Umma ya mwaka 2014 na kanuni zake.
 
Alisema kutokana na ukubwa wa upotevu huo wa fedha, hatua itakayofuata ni kuundwa kwa bodi ya uchunguzi ambayo itakuwa na watu wanne watakaoteuliwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango.
 
Alisema azma ya serikali ni kuimarisha utawala bora na kuimarisha usimamizi wa fedha za umma, hivyo watendaji wote wanapaswa kufahamu kuwa azma hiyo inatekelezwa bila ya kuyumba wala kumuonea haya mtu yeyote.

Hakuna Uhamisho Wanafunzi Wapya wa Kidato cha Tano

0
0

SERIKALI imesema shule zote zenye nafasi za wanafunzi wa kujiunga na kidato cha tano mwaka huu, zimejaa hivyo hakuna nafasi ya mwanafunzi kubadilishiwa shule au mchepuo aliochagua.

Hayo yalibanishwa jana katika taarifa iliyotolewa jana kwa vyombo vya habari mjini hapa na Msemaji wa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Rebecca Kwandu.
 
Kwandu alisema baada ya serikali kutangaza wanafunzi waliojiunga na kidato cha tano, baadhi ya wazazi na wanafunzi wamekuwa wakifika ofisi za Tamisemi kuomba kubadilishiwa shule au tahasusi (michepuo) walizochaguliwa.
 
“Tunapenda kuwaarifu kwamba shule zote zenye nafasi za wanafunzi wa kujiunga na kidato cha tano mwaka 2016 zimejaza, hivyo hakuna kinachoweza kubadilishwa,” alisema Kwandu.
 
Aidha, Kwandu alisema vigezo ambavyo vilitumika katika uchaguzi huo ni pamoja na ufaulu na uchaguzi wa wanafunzi wenyewe juu ya masomo wanayopenda kuendelea nayo kidato cha tano na sita.
 
“Kulingana na utaratibu uliowekwa na serikali, mwanafunzi mwenye sifa za kuchaguliwa kuendelea kidato cha tano na vyuo vya ufundi ni yule ambaye ufaulu wake ni kuanzia daraja la kwanza hadi la tatu. Wanafunzi hao wamepangwa kulingana na ufaulu wao masomo waliyochagua na nafasi zilizopo,” alisisitiza.
 
Pia alisema nafasi za shule walizopangiwa wanafunzi zimezingatia miundombinu ya shule husika na uwezo, na kwamba kila shule imepewa wanafunzi kulingana na nafasi zilizopo, hivyo hakutakuwa na nafasi ya kuwabadilisha kutoka shule moja kwenda nyingine kwa sasa.
 
Kutokana na hali hiyo, aliwataka wanafunzi wote waliochaguliwa kujiunga na kidato cha tano na vyuo vya ufundi kuripoti katika shule na vyuo walivyopangiwa kama walivyoelekezwa.
 
Alisema mwanafunzi ambaye hataripoti ifikapo Julai 24, ambayo ni tarehe ya mwisho kwa muda uliopangwa, atakuwa amepoteza nafasi yake kwa kuwa itachukuliwa na mwanafunzi mwingine ambaye hakupata nafasi awali.

UKAWA Watishia Kumpeleka Rais Magufuli Katika Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC)

0
0

Wabunge wa Ukawa wamemtaka Rais John Magufuli kutoa tamko juu ya uvunjifu wa haki za binadamu Zanzibar na kwamba wana mpango wa kumpeleka katika Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC) wakidai yanayotokea visiwani humo yana baraka zake. 

Katika mkutano wao na wanahabari jana, wabunge hao wamemtaka Waziri wa Mambo ya Ndani, Mwigulu Nchemba kwenda Zanzibar kujionea hali halisi badala ya kupata taarifa kutoka kwa wasaidizi wake. 

Hata hivyo, CCM imesema kuwa inalaani tamko hilo na kuwa kama Ukawa wanaona kuna masuala yanayohitaji kurekebishwa na kuhitaji hatua za haraka za Serikali watumie vyombo vinavyotambulika kisheria kama Bunge badala ya kuishia kulalamika “vichochoroni”. 

Akitoa tamko la wabunge hao jana, Mbunge wa Vunjo (NCCR-Mageuzi) alieleza kuwa hali ya kiusalama inazidi kuwa mbaya Pemba na Unguja baada ya uchaguzi wa marudio wa Machi 20 kutokana na baadhi ya wananchi kupigwa na vikosi alivyodai ni vya usalama. 

Mbatia alisema kuwa vikosi vya ulinzi hususani jeshi la polisi vimekuwa vikishiriki katika vitendo vya ukiukwaji wa haki za raia Pemba kwa zaidi ya miezi miwili kwa polisi kupiga mabomu ya machozi, kuwakamata ovyo wananchi, kuwapiga na kuwatesa na kisha kuwafungulia mashtaka bandia. 

Kutokana na vitendo hivyo, Mbatia alisema wabunge wa Ukawa wanapenda kusikia kauli ya wazi ya Dk Magufuli juu ya uonevu huo uliodumu kwa muda mrefu dhidi ya Wazanzibari na kutoheshimiwa haki za binadamu zikiwamo za kutoa maoni na kujikusanya. 

Mbatia, ambaye ni Mwenyekiti Mwenza wa Ukawa, alisema Rais anapaswa kutimiza wajibu wake kuhakikisha usalama wa raia kama anavyotakiwa kikatiba na kuhakikisha polisi wanawalinda wananchi na siyo kuwaonea. 
 
“Ukawa inasema wazi kuwa inaendelea kukusanya taarifa za vitendo vya ubakaji wa demokrasia na haki za binadamu ili kupata ushahidi wa kutosha wa kumfikisha Dk Magufuli ICC akajibu makosa hayo,” alisema Mbatia. 

Katika mkutano huo uliohudhuriwa na wabunge 66 waliosaini tamko hilo, Mbatia alisema Ukawa inamtaka Mkuu wa Jeshi la Polisi, IGP Ernest Mangu kuitoa amri ya kusitishwa kwa matendo hayo na achukue hatua dhidi ya askari wake ambao huwatesa raia ili kurudisha imani kwa wananchi. 

Alisema wananchi wa Pemba na Unguja waendelee kuikataa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kwa amani na pia wadumishe utaratibu wa kuheshimu sheria na kujizuia kufanya vitendo vya kukinzana na sheria. 

Lakini alipotakiwa kuzungumzia tamko hilo, Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Vuai Ali Vuai alitupa lawama zote kwa Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad. 

Alisema kuwa ndiye adui mkubwa wa Ukawa baada ya kususia uchaguzi wa marudio na kuhamasisha wananchi wasiitambue Serikali na sasa wafuasi hao wanatekeleza maagizo hayo kwa kukata mazao na kuleta fujo kwa wananchi wenzao. 

“Kazi ya dola ni kuhakikisha mtu havunji amani. Watu wanaofanya vitendo hivyo washughulikiwe ipasavyo na vyombo vya dola,” alisema Vuai. 

Alisema hakuna sababu ya kumpeleka Rais Magufuli katika mahakama ya ICC kwa kuwa anafanya kazi nzuri ya kuongoza nchi na kwamba kauli zilizotolewa na Ukawa ni za kitoto. 

Alivisihi vyombo vya dola kuendelea kuimarisha usalama visiwani humo ili watu wenye nia mbaya wasizoroteshe amani kutokana na matakwa ya viongozi wao. 

Awali katika mkutano huo, Mbunge wa Malindi (CUF), Ally Saleh alisema wameamua kutoa tamko hilo kutokana na hali kuzidi kuzorota Pemba na kwamba ni lazima Serikali itekeleze wajibu wake kuzuia machafuko zaidi. 

Kuhusu mipango yao ya kumshtaki Rais, alisema kesi hiyo haina haraka kwa kuwa hata wajukuu zao wanaweza kuifungua kwa kuwa makosa ya jinai hayafi. 

“Baada ya kukusanya ushahidi wa kutosha na kujiridhisha kufanya hivyo, tutafanya. Tanzania siyo kisiwa ulimwengu mzima unaangalia nini kinaendelea Zanzibar, hivyo tusipowajibika, dunia itatuwajibisha,” alisema Saleh. 

Mbunge wa Chambani (CUF), Yusuph Salim Hussein alisema vyombo vya usalama vimekuwa vikiwatuhumu wafuasi wa CUF kufanya vurugu hizo lakini tangu zianze tuhuma hizo hakuna mtu hata mmoja aliyewahi kushtakiwa kwa uharibifu mali au fujo. 

“Tangu mwaka 1992 hizo tuhuma kuwa sasa hakuna mtu aliyewahi kushtakiwa mahakamani na kutiwa hatiani. Ni wao (Serikali) ndiyo wanawaonea wananchi,” alisema. 

Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Hamad Yusuph Masauni alisema ni jambo la kusikitisha kuona viongozi wanawalinda wahalifu badala ya kuhimiza amani na usalama. 

Masauni alisema baada ya uchaguzi wafuasi wetu ndiyo wanafanya fujo hadi Machi 20 hali ilikuwa shwari Pemba laki ni viongozi wa CUF ndiyo chanzo cha matukio ya uhalifu unaoendelea Pemba baada ya Maalim Seif kwenda visiwani huko na kuwataka wasiitambue Serikali. 

“Hivi kabla ya tamko la Maalim Seif vikosi vya ulinzi na usalama havikuwapo ili vikakate mikarafuu na kuchoma nyumba za watu? Askari wetu wamefunzwa vizuri, wamekula kiapo kulinda usalama wa raia wote bila kujali chama,” 

Alisema nchi haiwezi kuendeshwa kwa kuacha watu wavunje amani na kwamba vyombo vya usalama vitamshughulikia mtu yeyote atakayekiuka sheria bila kujali chama.

Rais Magufuli Aeleza Sababu ya Kutengua Uteuzi wa Mkuu wa Wilaya Ya Ikungi

0
0

Juni 26 mwaka huu Rais John Pombe Magufuli alitangaza kuteua Wakuu wa Wilaya zote nchini, na Wakuu wa Mkoa watatu. Kati ya Wakuu wa Wilaya 139 walioteuliwa, 39 wamebakishwa katika nafasi zao huku 100 wakiwa ni wapya.

Katika hali ya kushangaza siku moja baada ya orodha hiyo kutangazwa, Rais Magufuli ametengua uteuzi wa mkuu wa wilaya ya Ikungi iliyopo mkoani Singida. Rais Magufuli alitengua uteuzi wa Bwana Fikiri Avias Said ndani ya masaa 24 tangu uteuzi wake.

Sababu kuu ya Rais kutengua Uteuzi huu ameisema leo hii wakati wa hafla ya kuwaapisha Wakuu wote walioteuliwa, ni kwamba jina lilikosewa, na kusema kwamba Mkuu wa Wilaya halali wa Ikungi ni Bwana Miraji Mtaturu ambaye ni Katibu wa Chama cha Mapinduzi (CCM) mkoa wa Mwanza,

Alichokiandika Rais Magufuli kuhusu ugunduzi wa gesi ya Helium nchini Tanzania

0
0
Jana ziliripotiwa taarifa kuwa watafiti kutoka chuo kikuu cha Oxford na kile cha Durham kwa ushirikiano na wataalamu wa madini kutoka Norway wamegundua uwepo wa takriban futi bilioni 54 za hifadhi kubwa zaidi duniani ya gesi adimu zaidi ya Helium nchini Tanzania.

Leo June 29 2016 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, John Pombe Magufuli kupitia account yake ya twitter amepost akizungumzia ugunduzi huo huku akitoa wito kujipanga katika eneo la mikataba.

"Tunamshukuru Mungu Tanzania tumegundua gesi aina ya Helium(He),wito wangu kwa wachumi,wanasheria na watanzania wote kwa ujumla tujipange

"Ugunduzi huu utuelekeze kujipanga hasa ktk eneo la mikataba yetu ili rasilimali hii adimu isaidie kuujenga uchumi wetu"

Mahakama Kuu Arusha Yatengua ushindi wa Mbunge wa Longido, Onesmo Ole Nangole (CHADEMA), yaamuru kurudiwa uchaguzi katika jimbo hilo.

0
0

Kesi iliyokuwa inaunguruma kuanzia tarehe 29.02.2016 katika mahakam kuu jijini Arusha imetolewa hukumu leo hii

Katika shauri hilo aliyekuwa mgombea ubunge wa CCM jimbo la Longido Dr KIRUSWA alifikisha mahakamni shauri hilo la kupinga matokeo ya ushindi dhidi ya mbunge wa Longido mh ONESMO NANGOLE

Akisoma hukumu hiyo,Jaji MWAGESI alisema kwamba mlalamikaji ndugu Kiruswa aliwakilishwa na Wakili Dr.Masumbuko Lamwai na Wakili Haraka.

Katika shauri hilo,dai la msingi la mlalamikaji bwana Kiruswa lilikua ni
1.Kutumika kwa lugha ya matusi na kashfa wakati wa kampeni kutoka kwa mh Onesmo Nangole
2.Kuwepo kwa wapiga kura kutoka nchi jirani ya Kenya walioletwa na Mh Nangole
3.kutumika kwa magari ya Chadema kwenye kusindikiza na kubebea masanduku ya kupigia kura
4.Mkurugenzi wa Uchaguzi kutangaza matokeo baada ya mgombea wa CCM kutolewa nje.
5.kutokea kwa vurugu ndani ya chumba cha kuhesabu matokeo

Kutokana na madai hayo na kwa kuzingatia kanuni,sheria na ushahidi uliotolewa pamoja na vielelezo na mashahidi wa pande zote mbili,Jaji kutoka mahakama kuu Bukoba Mh.Jaji Mwagesi alisema;
 
“Kutokana na kuzingatia viini vyote vya shauri hili kama vilivyosikilizwa na kwa mujibu wa sheria,Natamka kwamba;

Mahakama hii imetengua shauri hili na kwa kujirisha kwamba mchakato mzima haukuwa wa haki."

Taarifa: Rais Magufuli Awaapisha Wakuu wa Mikoa Watatu Aliowateua

0
0
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli leo tarehe 29 Juni, 2016 amewaapisha wakuu wa Mikoa watatu aliowateua Jumapili iliyopita tarehe 26 Juni, 2016.

Wakuu wa Mikoa walioapishwa leo Ikulu Jijini Dar es salaam ni Dkt. Binilith Satano Mahenge ambaye ni Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Dkt. Charles Ogesa Mlingwa ambaye ni Mkuu wa Mkoa wa Mara na Bi. Zainab Rajab Telack ambaye ni Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga.

Hafla ya kuapishwa kwa wakuu hao wa Mikoa imehudhuriwa na Makamu wa Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa, wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama na wakuu wa wilaya wateule ambao waliteuliwa na Rais Magufuli Jumapili iliyopita tarehe 26 Juni, 2016.

Aidha, miongoni mwa wakuu wa wilaya 139 walioteuliwa, Rais Dkt. John Pombe Magufuli amefanya mabadiliko madogo katika wilaya tatu ambapo ametengua uteuzi wa Mkuu wa Wilaya ya Rombo Mteule Mhe. Fatma Hassan Toufiq na badala yake amemteua Bi. Agness Elias Hokororo kuwa Mkuu wa Wilaya hiyo, ametengua uteuzi wa Mkuu wa wilaya ya Serengeti Mteule Bw. Emile Yotham Ntakamulenga na badala yake amemteua Bw. Nurdin Hassan Babu kuwa Mkuu wa Wilaya hiyo na ametengua uteuzi wa Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mteule Bw. Fikiri Avias Said na badala yake amemteua Bw. Miraji Mtaturu kuwa Mkuu wa wilaya hiyo.

Akizungumza katika hafla hiyo, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amewataka wakuu wa wilaya wateule kwenda kuchapa kazi na kutatua kero za wananchi katika wilaya zao huku wakizingatia kufanya kazi kwa uadilifu na uaminifu.

Rais Magufuli pia amewataka kusimamia ukusanyaji mapato ya serikali na matumizi ya fedha na rasilimali nyingine za umma, kuhakikisha wananchi wapo salama na pia kuhakikisha wananchi wanafanya kazi za uzalishaji mali.

“Katika kazi hizi wapo watakaowakejeli, katika kazi hizi wapo watakaowadhihaki, nyinyi kavumilieni na mmuweke Mungu mbele na mkawaweke watanzania mbele, mkafanye kazi kadiri Mungu atakavyokuwa amewaongoza.

“Nataka kuwahakikishia tunawaunga mkono kwa nguvu zote, mkafanye kazi bila uwoga wowote, katembeeni kifua mbele, kwa sababu tumewaamini wala msiwe na wasiwasi, ukifanya kitu kizuri kwa dhamira yako iliyo njema kitazaa matunda mazuri, ukifanya kitu kwa unafiki hakitafanikiwa” Amesema Rais Magufuli

Katika hafla hiyo, wakuu wa mikoa walioapishwa na wakuu wa wilaya wateule wamekula kiapo cha ahadi ya uadilifu kwa viongozi wa umma, zoezi ambalo limeongozwa na Kamishna wa Maadili Jaji Mstaafu Salome Kaganda.

Katika hatua nyingine, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amekutana na kufanya Mazungumzo na mwenyekiti mwenza wa taasisi ya Bill and Melinda Gates ya Marekani Bi. Melinda Gates ambapo Rais Magufuli amemuhakikishia mwenyekiti mwenza huyo kuwa serikali ya awamu ya tano itaendeleza na kuimarisha zaidi uhusiano wake na taasisi hiyo ambayo imekuwa ikishirikiana na Tanzania katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya Afya, Uongozi na Kilimo.

Kwa upande wake Bi. Melinda Gate amempongeza Rais Magufuli kwa kazi kubwa anayoifanya katika kukabiliana na rushwa na kuongeza ukusanyaji wa mapato ya serikali, na pia kwa nia yake thabiti ya kuinua sekta ya kilimo inayotegemewa na idadi kubwa ya watanzania na ameahidi kuwa taasisi ya Bill and Melinda Gates itaendelea kushirikiana na Serikali ya awamu ya tano katika kuongeza tija ya uzalishaji wa mazao ya kilimo.

Gerson Msigwa
Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano, IKULU
Dar es salaam
29 Juni, 2016

Waziri Mkuu Aagiza Wakuu wa Wilaya na Mikoa kutembelea Vijijini ili kujua matatizo ya wananchi.

0
0

Na Daudi Manongi
Waziri Mkuu Mhe.Kassim Majaliwa ameagiza wakuu wa wilaya na mikoa kufanya ziara katika maeneo yao hasa vijijini ili kujua matatizo ya wananchi wao kwa ukaribu na kuyapatia ufumbuzi.
 
Mhe.Majaliwa ameyasema hayo leo hii Ikulu jijini Dar es Salaam wakati wakuu wa wilaya na mikoa walipokuwa Ikulu wakila kiapo cha maadili ya viongozi kabla ya kwenda kuapishwa na wakuu wa mikoa yao.
 
Aidha Waziri Mkuu amesema kuwa  wakuu wa mikoa na wilaya waache kukaa maofisini mwao badala yake watembelee wananchi na hasa wale wa hali ya chini ili kujua matatizo yao ya Ardhi na kupatia ufumbuzi migogoro ya wafugaji na wakulima.
 
Pia Mhe.Majaliwa amewasisitiza wakuu hao kutambua kwamba majukumu waliyonayo ni makubwa na wananchi wana mategemeo makubwa juu yao na hivyo ni  budi wakatekeleza wajibu wao na kuhakikisha watanzania wanapata huduma zote za muhimu kwa kutumia elimu, uwezo, uadilifu, uaminifu na uwajibikaji walionao ili kufanikisha maendeleo kwa wananchi.
 
Aliongeza kuwa wakuu hao wana jukumu kubwa la kusimamia pesa za serikali pesa za miradi zinakokwenda katika halmashauri za wilaya zao na kukazia kuwa Serikali haitasita kuchukua hatua kwa yeyote ambaye hatofanya kazi zake kikamilifu.
 
Waziri mkuu amewaagiza wakuu wa Mikoa kushirikiana kwa karibu na wakuu wa Wilaya ili kutafuta ufumbuzi wa matatizo ya maeneo yao kwani wananchi wana kiu ya maendeleo katika maeneo yao.

Makamu wa Rais awataka wakuu wa wilaya na mikoa kukamilisha zoezi la madawati kabla ya June 30.

0
0
Makamu wa Rais Mhe Samia Suluhu amewataka wakuu wa wilaya na mikoa kuhakikisha wanamaliza zoezi la upatikanaji wa madawati kwa shule za msingi na sekondari.

Mhe. Suluhu ameyasema hayo leo Ikulu Jijini Dar es Salaam wakati wakuu wa wilaya na mikoa walipokuwa Ikulu wakila kiapo cha maadili ya viongozi kabla ya kwenda kuapishwa na wakuu wa mikoa yao.

Aidha amewaagiza viongozi hao kusoma alama za nyakati kwa kuangalia makosa ya waliokuwepo kabla yao ili kuhakikisha hawarudii makosa yaleyale.

Mhe.Suluhu pia amesema kuwa Serikali haitaki kusikia wananchi wanalia njaa na hivyo wakuu wa wilaya wahakikishe chakula kinapatikana katika maeneo yao kwani hilo ni jukumu lao.

Aliongeza kuwa wakuu wa wilaya wana majukumu makubwa ya kuhakikisha wananchi wanapata huduma zote za muhimu katika maeneo yao kwani wananchi wana mategemeo makubwa juu yao.

Aidha ameagiza wakuu wa Wilaya hao kufanya kazi karibu na Maafisa Tarafa ili kujua kero za wananchi na kuzifanyia kazi kwa kasi ili wananchi wafaidike na maendeleo yawafikie kwa haraka.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), George Simbachawene  ivi karibuni aliwaagiza wakua wa wilaya na mikoa kuhakikisha wanatimiza agizo la Rais John Pombe Magufuli kuhakikisha hakuna mwanafunzi atakayekaa chini kwa uhaba wa madawati kufikia June 30,2016.

Tundu Lissu Awekwa Rumande Kwa Kukosa Dhamana.

0
0
MBUNGE wa Singida Mashariki, Tundu Lissu (Chadema) jana alijisalimisha Kituo Kikuu cha Polisi, Dar es Salaam kwa ajili ya kuhojiwa kutokana na kauli za uchochezi alizozitoa, lakini akakosa dhamana.

Hatua ya Lissu kukosa dhamana na kulala rumande imekuja siku moja baada ya kuachiwa kwa dhamana katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu anakokabiliwa na mashitaka ya kuchapisha taarifa za uchochezi katika gazeti la Mawio.

Alifika kituoni hapo jana saa 7.38 mchana akiwa katika gari aina ya BMW lenye namba za usajili T549 BHH na kuhojiwa kwa saa tatu mfululizo juu ya kauli yake ya kumuita Rais John Magufuli kuwa ni dikteta ‘uchwara’, kuandika uchochezi katika mitandao ya kijamii na kutoa kauli za kuudhi.

Kwa mujibu wa Mwanasheria wa Lissu, John Mallya, kilichomfanya Lissu alale rumande ni kutokana na polisi kudai kuwa amefanya uchochezi na kutumia lugha ya kuudhi ya kusema kuna mtu anaitwa dikteta uchwara.

“Lissu amezungumza msingi wa kwa nini amesema dikteta uchwara kwenye mahojiano yake na amerekodiwa katika nyaraka za kipolisi na amehojiwa kwa saa tatu kuhusu jambo hilo, na kauli aliyosema jana kutoka mahakamani,” alisema Mallya.

Alisema wao kama wanasheria wataendelea kumpigania Lissu na kama atafikikishwa mahakamani leo watakuwepo kuhakikisha anapata haki zake zote za kisheria. Mallya alidai hakuna ujumbe wowote alioandika Lissu uliokuwa unasababisha uchochezi.

Awali, Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema ambaye alikuwepo kituoni hapo, alidai hakuna jambo baya ambalo wanaona Lissu kalizungumza, bali alichokifanya ni kusema mtazamo wake kwa jinsi anavyoona.

Alisema chama hicho kitaendelea kuikosoa serikali pale kitakapoona mambo hayaendi sawa ili kuhakikisha serikali inasimama katika hali ambayo kila mmoja ataridhishwa nayo.

Juzi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Lissu aliachiwa kwa dhamana katika kesi ya inayomkabili ya mashitaka ya kuchapisha taarifa za uchochezi katika gazeti la Mawio, akijumuishwa kwenye kesi hiyo akiwa na washtakiwa wenzake ambao ni mwandishi wa habari hizo, Jabir Idrissa, Mhariri wa gazeti hilo, Simon Mkina na Mchapishaji wa Kampuni ya Jamana, Ismail Mehboob.

Habari Zilizopo Katika Magazeti ya Leo Alhamisi ya June 30

Polisi Yaua Majambazi Matatu Yaliyokuwa Yamejificha Katika Mapango ya Ambano

0
0
POLISI mkoani Tanga imewaua watu watatu katika mapigano ya risasi wanaodaiwa kuhusika katika mauaji ya watu jijini humo wakiwamo watu wanane waliochinjwa katika Kitongoji cha Kibatini, Kata ya Mzizima.

Limewahakikishia wananchi kwamba eneo la Amboni yakiwemo Mapango ya Majimoto yanayodaiwa kutumiwa na wahalifu waliosababisha mauaji hasa ya wakazi wanane wa Kibatini lipo salama, baada ya watuhumiwa wengine watatu na silaha mbalimbali kukamatwa juzi.

Waliokamatwa ni Abdulkarim Singano, Seif Jumanne na Ramadhani Mohamed ambao baadaye walikufa kutokana na majeraha ya risasi wakati wa mapigano katika msitu wa Kibatini wakati askari wakijaribu kuwadhibiti, siku moja baada ya Abuu Seif anayedaiwa kuwa kiongozi wao kuuawa jijini Dar es Salaam.

Silaha zilizokamatwa ni bunduki mbili aina ya SMG, bastola moja, risasi 30, mapanga, majambia ambavyo vimepatikana kupitia msako ulioshirikisha kikosi kazi cha vyombo vya ulinzi na usalama vilivyohusisha askari kutoka majeshi yote.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga, Leonard Paulo alibainisha hayo wakati akitoa taarifa ofisini kwake jana kwamba, wahalifu hao walikamatwa Juni 28, mwaka huu wakati askari walipokuwa katika harakati za kuwakamata kwenye msitu wa Kibatini jirani na mapango ya Majimoto, Kata ya Mzizima jijini Tanga.

“Majambazi waliohusika kuua wananchi wanane pale Kibatini ndio tumewakamata lakini kwa bahati mbaya watatu kati yao wamekufa wakati wakidhibitiwa na askari,” alisema Kamanda Paulo. 

Alisisitiza wameyakagua yaliyokuwa maficho yao na kujiridhisha kuwa Amboni iko salama na imedhibitiwa.

Mapema wiki hii, Polisi wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, walitangaza kumuua Abuu Seif aliyeshiriki katika mauaji ya Tanga, baada ya kumpiga risasi alipokataa kujisalimisha baada ya kubainika kujificha katika nyumba moja jijini Dar es Salaam. Alifariki dunia akipelekwa hospitali.

Shule Kongwe 88 Kufanyiwa Ukarabati

0
0

SERIKALI ya Awamu ya Tano imetenga Sh bilioni 33 kwa ajili ya mpango maalumu wa ukarabati mkubwa na uboreshaji wa miundombinu mbalimbali, yakiwemo majengo ya madarasa, mabweni na nyumba za walimu katika shule kongwe za sekondari za serikali nchini.

Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi, Profesa Joyce Ndalichako, alisema hayo wakati wa uzinduzi rasmi wa mpango huo katika Shule ya Sekondari ya Mzumbe iliyopo Wilaya ya Mvomero mkoani Morogoro.

Profesa Ndalichako alisema mpango huo wa miaka miwili utahusisha shule kongwe 88 za serikali kwa kufanyiwa ukarabati mkubwa wa miundombinu, majengo ya madarasa, nyumba za walimu, mabweni, majengo ya chakula na uboreshaji wa maabara na vitendea kazi vyake.

Waziri huyo alikuwa pia mgeni rasmi kwenye maadhimisho ya Siku ya Elimu Tanzania iliyofanyika juzi kwenye Ukumbi wa Shule ya Sekondari Mzumbe na kuhudhuriwa na wadau wa sekta ya elimu wakiwemo wakuu wa shule za sekondari za serikali na maofisa elimu wa mikoa kutoka mikoa yote ya Tanzania Bara.

Alisema utekelezaji wa mpango huo unatarajia kuanza wakati wotote baada ya kupitishwa kwa Bajeti ya Serikali na kuanza kutumika na utaanza kwa awamu ya kwanza ambako shule kongwe 33 zitahusika.

“Tumekadiriwa kuwa kila shule itagharimu shilingi bilioni moja na kwa maana hiyo shule 33 zimeingizwa awamu ya kwanza. Fedha hiyo inaweza ikapungua kulingana na mazingira ya kitadhimini ya uchakavu wa majengo,” alisema Profesa Ndalichako.

Alisema uboreshaji wa elimu ni pamoja na ubora wa majengo na miundombinu mingine katika shule hizo, na lengo la kuzirejesha katika uhalisia wake wa zamani wa kuwa na mandhari nzuri za kuvutia wanafunzi, walimu na wazazi.

“Shule hizi tumeziweka katika mpango maalumu wa miaka miwili kukarabatiwa majengo yake, miundombinu ya kufundishia, vifaa vya kila somo, vitabu vya kufundishia na kujifunzia, vifaa vya kutosha vya maabara na kuboresha makazi ya walimu,” alifafanua Profesa Ndalichako.

Naye Mkurugenzi wa Usimamizi wa Elimu Ofisi ya Rais Tamisemi, Juma Kaponda, alimpongeza Waziri Ndalichako kwa kusimamia uboreshaji wa shule kongwe za sekondari na kuomba wadau mbalimbali waliosoma shule kongwe hizo na wanazo nyadhifa kubwa serikalini na sekta binafsi kuona wanao wajibu wa kuchangia maboresho hayo.

Gesi Iliyogunduliwa Tanzania Yazua Mjadala Mzito

0
0

Wakati Rais John Magufuli akiungana na Watanzania wengine wanaofurahia kugunduliwa kwa gesi ya helium nchini, baadhi ya wataalamu wa miamba wameshauri uchunguzi zaidi ufanyike ili kuthibitisha uwepo wa kiasi hicho.

Juzi, kulikuwa na taarifa za watafiti kutoka Chuo Kikuu cha Oxford na kile cha Durham kwa ushirikiano na wataalamu wa madini kutoka Norway kuwa wamegundua uwepo wa takriban futi 54 bilioni za ujazo za hifadhi kubwa zaidi duniani ya gesi adimu zaidi ya helium katika Bonde la Ufa, Kusini mwa Tanzania.

Katika ukurasa wake wa Tweeter, Dk Magufuli alisema ni jambo la kumshukuru Mungu huku akiwataka wachumi, wanasheria na Watanzania kwa ujumla kujiandaa.

“Tunamshukuru Mungu Tanzania tumegundua gesi aina ya helium, wito wangu kwa wachumi, wanasheria na Watanzania wote kwa ujumla tujipange. Ugunduzi huu utuelekeze kujipanga hasa katika eneo la mikataba yetu ili rasilimali hii adimu isaidie kuujenga uchumi wetu,” alisema.

Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo alikaririwa akithibitisha ugunduzi huo na kusema Serikali itaitumia gesi hiyo vizuri.

Hata hivyo, akizungumzia utafiti huo, Mkurugenzi wa Taasisi ya Utafiti wa Miamba (Geological Survey of Tanzania), Profesa Abdulkarim Mruma alisema hawakushiriki kwenye utafiti huo, hivyo ni mpaka wafanye utafiti wao kuthibitisha.

“Kwanza tulikuwa na mradi wa kutafuta helium na Wajerumani na tuliainisha maeneo yanayoweza kupatikana. Kwa hiyo hao watatifi walikuja kufuatilia maeneo tuliyoyaweka, ila hatukwenda nao,” alisema.

“Unajua mara nyingi watafiti wa madini huwa wana tabia ya kutaja viwango vikubwa vya upatikanaji wa madini ili kuongeza hisa za kampuni zao kwenye masoko ya madini. Kwa hiyo tutafuatilia kwa kuchimba ili kuhakikisha kama kweli hicho kiwango walichosema kipo. Kama hakipo tutawaeleza,” alisema Profesa Mruma.

Alisema gesi ya helium imekuwa ikipatikana kwa kiasi kidogo nchini tangu wakati wa ukoloni, lakini ugunduzi wa sasa ni mkubwa kidunia. 

Mkurugenzi wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), Dk James Mataragio alisema hawana taarifa rasmi ya ugunduzi huo, hivyo hawezi kusema Taifa litafaidikaje.

“Tangu jana (juzi) tumeona vyombo vya habari vimeandika kuhusu gesi hiyo. Ukweli ni kwamba sijapokea taarifa rasmi kuhusu ugunduzi huo. Uchimbaji wa gesi ya helium ni tofauti kidogo na gesi nyingine, ni mpaka ithibitishwe kwanza na wataalamu kama ipo kweli ndipo tujue tutafaidikaje,” alisema.

Mkuu wa Idara ya Jiolojia ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk Elisante Mshiu alisema kama kweli kiasi hicho cha gesi kipo, Tanzania itakuwa na gesi hiyo mara mbili kuliko inayopatikana kote duniani.

Dk Mshiu alisema gesi hiyo inayopatikana maeneo mbalimbali duniani ina mita za ujazo 25 bilioni, hivyo iliyopo Tanzania ni mara mbili yake.

Akizungumza kupitia mtandao wa ABC, mmoja wa wanasayansi Profesa Chris Ballentine kutoka Chuo Kikuu cha Oxford cha Uingereza alisema gesi hiyo iliyogunduliwa inaweza kutumika kwa zaidi ya miaka 20 ijayo.

Profesa Ballentine anayefanya kazi na kampuni ya Norway ya kutafuta helium, alisema ni mara ya kwanza kuitafuta helium na kuipata kwani mara nyingi hupatikana kwa bahati tu.


Mvutano Mkali Waibuka Wakati wa Kupitisha Muswada wa Marekebisha ya sheria ya Ununuzi wa Umma wa Mwaka 2016

0
0

Serikali imejikuta katika wakati mgumu wakati wa upitishaji wa Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Ununuzi wa Umma wa mwaka 2016 baada ya wabunge kupinga baadhi ya hatua zilizochukuliwa katika muswada huo. 

Jana, Bunge lilitumia zaidi ya saa mbili kupitisha muswada huo huku mvutano ukiibuka katika nyongeza ya mapendekezo ya ununuzi wa dawa na vifaatiba kufanywa kwa dharura na kupinga kwa kamati za fedha na mipango kuondolewa katika kusimamia mchakato wa zabuni kwenye halmashauri. 

Mashambulizi hayo yaliongozwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti, Hawa Ghasia na wabunge Joseph Kakunda (Sikonge CCM), Profesa Anna Tibaijuka (Muleba Kusini CCM) na Andrew Chenge wa Bariadi Magharibi (CCM), kiasi cha kumfanya Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), George Masaju kukubali baadhi ya mapendekezo ya Bunge kwa shingo upande. 

Hii ni mara ya kwanza kwa wabunge wa CCM kuipinga vikali Serikali kwa kura wakati wa kupitisha vifungu na kufanya Bunge lirudishe uhai wa mjadala tangu Ukawa waanze kususia vikao vinavyoendeshwa na Naibu Spika, Dk Tulia Ackson. 

Awali, katika mjadala wabunge wengi walipongeza hatua ya Serikali kupunguza muda na gharama za mchakato wa zabuni, ushirikishaji wa makundi maalumu katika jamii kwenye zabuni za umma lakini walipinga uamuzi wa kuwaondoa madiwani katika mchakato wa ununuzi. 

Katika kifungu cha 11 cha muswada huo, Serikali ilikusudia kuondoa jukumu la kamati ya fedha na mipango katika usimamizi wa masuala ya ununuzi ya halmashauri. 

Kabla ya Bunge zima kukaa kama kamati kupitisha muswada huo, Waziri wa Fedha, Dk Philip Mpango alieleza kuwa Serikali ilikuwa imeridhia kurudisha jukumu la kamati hizo ambazo huundwa na madiwani kuwasimamia watendaji watakaoshindwa kutekeleza kazi zao. 

Licha ya Serikali kukubali hoja hiyo, wabunge bado waliitaka kuingiza maana katika kifungu cha pili na kuweka maboresho kifungu cha 24 ili vifaatiba na dawa vinunuliwe kwa dharura huku Masaju akipinga kwa maelezo kuwa suala hilo lingeingizwa kwenye kanuni atakazotunga waziri. 

Ghasia alieleza kuwa vifaatiba na dawa ni muhimu katika kuokoa maisha ya binadamu hivyo ni vyema kianzishwe kifungu maalumu katika sheria badala ya kubaki katika kanuni na kusubiri majaliwa ya waziri. 

Kitendo cha Masaju kupinga pendekezo hilo, kiliwafanya wabunge, Chenge, Sophia Simba (Viti Maalumu) na Kangi Lugola wa Mwibara kusimama wakisema Serikali inataka kupitisha mambo kibabe. 

“Kila siku sheria zinakuwa mbaya kwa sababu maoni ya wabunge yanapuuzwa. Serikali ikitaka mambo yake yapite inalazimisha, haiwezekani. Dawa ni maisha, AG kubali hili na likileta shida mtaleta turekebishe mbona mengine huwa mnaleta tunarekebisha?” alisema Lugola. 

Chenge alisema Serikali ingekuwa imeipatia muda kamati ya bajeti imalize kazi zake, kusingetokea mvutano kwa kuwa mengine wangejadiliana na kuyamaliza. 

Mvutano huo ulimfanya Ghasia kuhamia kwenye meza ya Chenge ili kupata ushauri wa kisheria na hata wakati mwingine kusahau na kumweleza Naibu Spika kuwa baadhi ya masuala angeeleza mwanasheria wake (Chenge). 

Pamoja na Serikali kukataa mapendekezo hayo, wabunge walipigia kura ya ‘Ndiyo’ maboresho ya kamati na kuwaacha Masaju na Dk Mpango wakitikisa vichwa kwa masikitiko. 

Hoja nyingine iliyomfanya Masaju kususia kuendelea kutetea ni ile ya Profesa Tibaijuka iliyopitishwa na wabunge ya kuongeza maneno yatakayowataka wazabuni wa kimataifa kuhusisha wazawa katika kifungu cha 18 cha muswada. 

“Msitunge Sheria kwa hasira. Hiki kifungu kitakuwa kigumu kutekelezeka. Tungeni hivyo lakini mjue itakuja kuleta shida,” alisema Masaju akionyeshwa kukerwa na kilichofanywa na wabunge na kueleza maneno hayo tayari yalikuwapo kwenye Sheria ya Ununuzi ya mwaka 2011 inayoboreshwa. 

Sehemu nyingine iliyoleta mjadala ni pendekezo la Kamati ya Bajeti kuongeza kifungu cha kuanzisha akaunti maalumu ya ununuzi mdogo mdogo utakaozisaidia taasisi za umma kutumia wataalamu wa ndani na kununua vifaa vya marekebisho madogo kama kurekebisha vyoo na vitasa. 

Masaju alipinga pendekezo hilo akisema litafungua ufisadi katika halmashauri jambo ambalo wabunge wamekuwa wakilalamikia kila siku. 

Wabunge Wataka Clouds Tv Iadhibiuwe Kwa Kufanya Mahojiano na Kijana Ambaye ni SHOGA

0
0

WABUNGE wameiomba serikali kukichukulia hatua kituo cha televisheni, Clouds Tv nchini kwa kukiuka maadili na taaluma ya habari kwa kurusha kipindi ambacho maudhui yake yalikuwa ni kutangaza mapenzi ya jinsia moja.

Mbunge wa Viti Maalumu, Amina Mollel (CCM) aliomba Mwongozo kuhusu kurushwa kwa kipindi ambacho kilikuwa kikimhoji kijana mmoja ambaye anajihusisha na vitendo vya ushoga.

“Napenda kuweka maslahi yangu kuwa mimi mwenyewe ni mwanahabari na taaluma hii naifahamu na ndio maana nikaona ni vyema nisimame angalau kupata muongozo wako,” alisema Mollel na kuongeza kuwa sheria ya nchi hairuhusu ushoga kwa maana hiyo kama mwandishi wa habari alipaswa kuzungumzia ushoga, basi angeelimisha jamii kwa kuonesha kuwa kijana huyo anajutia kufanya vitendo hivyo.

Alisema mwandishi huyo angefanya hivyo ili kutoa taarifa kwa wengine kwamba vitendo hivyo sio vizuri katika jamii badala yake kipindi kilihamasisha vitendo vya ushoga na alionesha ni mtu anayefurahia kitendo kile, na jambo la kusikitisha asubuhi hii (jana), mwendeshaji wa kipindi hicho alialikwa katika kipindi cha asubuhi cha kituo hicho, badala ya kuomba radhi ameishia kujitetea.

Kutokana na maelezo hayo, aliomba Mwongozo wa Spika pamoja na Kanuni na kwa kuwa serikali ipo, itoe kauli kama inaruhusu ushoga au kama hairuhusu ni hatua gani inachukua kwa kituo hicho ili iwe fundisho kwa vingine.

Naye Mbunge wa Viti Maalumu, Agness Maro (CCM) alisema kijana huyo aliyehojiwa na Kipindi cha Take One cha Clouds Tv amewaaibisha wakazi wa Musoma mkoani Mara, hivyo aliiomba serikali imchukulie hatua kwa sababu anaweza kuwafundisha tabia zisizofaa vijana wengine.

Naibu Spika, Dk Tulia Ackson akijibu miongozo hiyo, alisema jambo hilo linapaswa kushughulikiwa kwa mujibu wa sheria zilizopo.

==> Msikilize shoga huyo akihojiwa

Milioni 800 Zatengwa Kuwasaidia Waathirika wa UKIMWI Nchini

0
0

ZAIDI ya Sh milioni 800 zinatarajiwa kukusanywa na Mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGM) kwa kushirikiana na Tume ya Taifa ya Kudhibiti Ukimwi (TACAIDS) kwa ajili ya kusaidia waathirika wa Virusi Vya Ukimwi mwaka huu.

Fedha hizo zitakusanywa kupitia kampeni maalumu ya kupanda mlima Kilimanjaro ijulikanayo kama Kill Challenge inayofanyika kwa mwaka wa 15, ambayo kwa mwaka huu wapanda mlima 100 wamejitokeza kushiriki.

“Mgodi wa Geita kwa kushirikiana na Tacaids unatarajia kupandisha watu 50 katika kilele cha mlima Kilimanjaro na kundi lingine la waendesha baiskeli 50 linataraji kuzunguka mlima huo kwa ajili ya kukusanya fedha hizo,” alisema Meneja Mawasiliano wa Mgodi wa GGM, Tenga Tenga.

Tenga alisema kampeni hiyo ya Kili Challenge inaongozwa na Balozi wake, Mrisho Mpoto ambaye ni msanii wa kughani mashairi na upandaji huo wa mlima utafanyika Julai 16 na kumalizika Julai 22, mwaka huu.

Alisema mgeni rasmi katika uzinduzi huo anatarajiwa kuwa Rais mstaafu wa Awamu ya Nne, Jakaya Kikwete, ambaye ataanzisha safari hiyo huku mapokezi ya kuwapokea wapandaji hao akiwa ni Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Said Mecky Sadiki.

Naye Mwakilishi wa Tacaids, Jackson Peter, alisema Kili Challenge ya mwaka huu imepata uzito wa kipekee kutokana na Umoja wa Mataifa (UN) kupitia Shirika lake la Maendeleo la (UNDP) kutoa wawakilishi wanane kushiriki upandaji mlima huo kwa ajili ya kusaidia watu walioathirika na Virusi Vya Ukimwi nchini.

Balozi wa Kili Challenge, Mpoto aliwataka wananchi na jamii kwa ujumla kutambua mapambano dhidi ya Ukimwi ni ya jamii yote hivyo inapaswa kuunga mkono jitihada za serikali kwa ajili ya kupambana ili kufikia sifuri tatu.

“Naamini kwamba jitihada zinazofanywa na mfuko huu zinahitaji kuungwa mkono na Watanzania wote na wadau wenye machungu na nchi hii, hivyo tuungane kila mmoja wetu ama kwa kuxchangia au kumuelisha mwenzake ili mapambano haya yalete mabadiliko,” alisema Mpoto.

Tangu kuanza kwa kampeni hiyo miaka 15 iliyopita zaidi ya Dola za Marekani 8,000 zimekusanywa na kugawiwa katika asasi mbalimbali nchini zinazoshiriki katika mapambano na kusaidia waathirika wa Ukimwi.

Fedha hizo zimepelekwa katika kusaidia mapambano dhidi ya Ukimwi, ikiwamo kujenga vituo vya ushauri na upimaji wa Ukimwi, ambavyo baadhi yao ni vile vilivyopo mkoani Tanga, Manyoni mkoani Singida na Geita.

RIWAYA: Mwanafunzi Mchawi ( A Wizard Student ) - Sehemu ya Saba

0
0
Mtunzi:  Enea Faidy


.....DOREEN alimkubalia Eddy kuwa mpenzi wake lakini alimweleza kuwa kuna sharti ambalo Eddy lazima alifuate ndipo awe nae.Dorice hakutaka kukubali kirahisi kumwachia Doreen kuwa na Eddy hivyo alipanga kulipiza ili Doreen asije kumsahau.Mwalimu John alipigwa na mkewe mpaka akapoteza fahamu ambapo mkewe alichanganyikiwa sana baada ya kumwamsha bila mafanikio....

Endelea.....
...MWALIMU JOHN alikuwa kimya pale kitini akiwa hana fahamu yoyote, mkewe akazidi kuchanganyikiwa sana kwani alihisi tayari mumewe ameaga dunia.

"Jamani mume wangu amka bado nakupenda! Nisamehe Mimi John wangu!" Alizidi kulia mke wa mwalimu John kwa huzuni na majuto makali. Alijiona mjinga sana kwa kujichukulia maamuzi mkononi bila hata kumdadisi vizuri.

Simanzi ilimtanda mwanamke yule bila kujua la kufanya, machozi yalichuruzika kama mito miwili usoni kwake kwani ndio kwanza ndoa yao ilikuwa changa kabisa tangu waoane miezi mitano iliyopita sasa iweje John aage mapema kiasi hicho? Mkewe aliufikiria upweke ambao angekabiliana nao Siku za usoni. Huzuni ikamzidia.

Mwalimu John akiwa bado ameyafumba macho yake akahisi yumo kwenye usingizi mzito sana lakini alikisikia vyema kilio cha mkewe.

Alitamani aamke ili amtulize mkewe lakini mwili ulikuwa kama umegandishwa na sumaku. Hakuweza hata kutikisika, ghafla akahisi upepo mkali sana ndani ya nyumba yake alipotazama ukutani akakutana na sura ya kutisha sana.

Huku ikifuka moshi mdomoni, macho mekundu kama damu na kichwani yalichomoza mapembe mawili marefu. John aliogogopa sana kwani tangu azaliwe hakuwahi kukutana na kiumbe wa ajabu na wakutisha namna ile. Alitamani azinduke usingizini lakini hakuweza, hivyo alibaki akitetemeka.

Ghafla kiumbe yule akabadilika na kuwa sura ya msichana mrembo sana. Mwalimu John akabaki kinywa wazi akistaajabu ya Mussa. Alipotazama vizuri aligundua ni Doreen , akashtuka sana.Doreen alimtazama mwalimu John kwa dharau sana kisha akaachia kicheko kikali sana.

"Mimi ni Doreen Mbwana! Daima usinichezee maana sichezewi kirahisi.. Unataka kuniendea Malawi we? Hahahahah umechelewa sana John, nina nguvu kuliko unavofikiria"

Doreen akamsogelea John, na kutoa kucha zake ndefu nyembamba kama msumari kisha akamgusa mdomo John."Umeniita Nimekuja! Sasa utaipata fresh...! Hahahahahahahhh" alisema Doreen kisha akatoweka . John alihema kwa nguvu sana huku woga ukiwa umemtawala kupita kiasi kwani maneno ya Doreen yalimtisha.

Rais Magufuli Amtumbua Mtu Aliyekuwa Akiiba Milioni 7 Kila Dakika Kwa Kushirikiana na TRA

0
0

RAIS Dk. John Magufuli amemtumbua mfanyabiashara mmoja maarufu Dar es Salaam, aliyebainika kufanya miamala ya fedha ya Sh milioni saba hadi nane kwa kila baada ya dakika moja.

Kutokana na hesabu ya Sh milioni saba anayoingiza kwa dakika moja, mfanyabiashara huyo hutengeneza Sh milioni 420 kwa kila saa moja, sawa na Sh bilioni 5.2 kwa saa 12 na Sh trilioni 16 kwa mwezi ambazo halipi Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT).

Rais Magufuli amesema mfanyabiashara huyo aliyebainika kuwa na makampuni mengi, alikuwa akishirikiana na Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni nchini (BRELA) pamoja na Mamlaka yaato Tanzania (TRA).

Mkuu huyo wa nchi alitoa kauli hiyo Ikulu, Dar es Salaam jana, baada ya kuwaapisha wakuu wapya wa mikoa watatu katika hafla iliyohudhuriwa pia na wakuu wa wilaya wateule.

Alisema waligundua jipu hilo baada ya kufuatilia kwenye mapato.

“Tulikuwa tunafuatilia kwenye ‘revenue’ (mapato), kwenye zile VAT ambazo zinatumika ‘ku-collect revenue’ (kukusanya mapato), yupo mtu mmoja ambaye alikuwa ametengeneza kampuni zake nyingi, alikuwa anafanya ‘transaction’ (miamala) ya fedha kila dakika moja kati ya Sh milioni saba na nane.

“Na hizo risiti alikuwa anaziuza kwa wafanyabiashara wengine, kwenye VAT anatakiwa kulipia kwa asilimia 18. Wafanyabiashara wengine hao walikuwa wanauziwa kwa asilimia tano na wakishauza bidhaa wanakwenda kuomba TRA iwarudishie hiyo asilimia 18, kwa hiyo Serikali imekuwa ikipoteza asilimia 18.5, ni matrilioni na matrilioni ‘of money’ (ya fedha).

“Bahati nzuri huyo mtu yuko kwenye mikono salama, tunafuatilia namna tutakavyorudisha hizo fedha, na huyo mtu alikuwa ana-connection kati ya watu wa BRELA na TRA… hiyo ndiyo Tanzania.

“Najaribu tu kutoa mfano ili katika maeneo yenu mkasimamie mapato ya Serikali, kwa sababu tumepoteza mapato mengi kuliko tunavyofikiria, huku Watanzania wakiteseka sana, na mambo yanayofanyika ni ya ajabu,” alisema Rais Magufuli akiwaambia wakuu hao wa mikoa na wilaya.

Pamoja na mambo mengine, Rais Magufuli alisema mchakato wa kupata wakuu wapya wa wilaya ulikuwa mgumu, na kwamba amewaacha wengi wa zamani kwa kuwa hawakutimiza vigezo alivyovitaka.

“Mchakato wa kupata ma-DC ulikuwa mgumu kwa sababu ilibidi tuangalie historia ya kila mmoja. Tuliangalia mambo mengi sana, lakini pia tuliangalia kwa ku-preview atatimiza haya tunayotaka kuyafanya kwa miaka mitano?

“Na ndiyo maana mnavyoona ma-DC wa zamani waliorudi ni 39, kwa hiyo wale 101 wote hawakurudi… niseme tu ukweli kwamba hawakufikia vigezo tulivyokuwa tunavitaka,” alisema Rais Magufuli.

Alisema katika uteuzi huo, alichukua wakurugenzi kwa kuwa walifanya vizuri katika maeneo yao waliyokuwa wakiyaongoza.

“Tulichukua wakurugenzi walio-perform vizuri katika maeneo yao. Wapya wako takribani 100 na waliobaki ni hao kati ya 38 na 39. Ni matumaini yangu kwamba mtakwenda kufanya kazi na kutimiza wajibu wenu.

“DC ni nafasi kubwa ya uongozi katika Serikali na ndiyo maana mfano mkubwa wa DC mstaafu ni Waziri Mkuu (Kassim Majaliwa), ni kwa sababu alitimiza wajibu wake na leo yuko hapa,” alisema.

Mkuu huyo wa nchi aliwapa mikakati ya kufanya kazi wakuu hao wa wilaya kwa kutimiza dhana ya kuchapa kazi kwa niaba ya Serikali.

“Nina matumaini makubwa mtakwenda kutimiza dhana ya kuchapa kazi kwa niaba ya Serikali, ninyi ndio wawakilishi wetu na ndio mnawakilisha wananchi wa maisha yote.

“Watanzania wana matatizo na changamoto kubwa. Ni matumaini yangu kwamba hamtaniangusha na hamtaiangusha Serikali. Nina imani mtakwenda kutatua matatizo ya wananchi, hasa walio masikini, sitegemei wala sifikirii kwamba mkawe chanzo cha kutengeneza matatizo,” alisema Rais Magufuli.

Kutokana na hali hiyo, aliwataka wasimamie haki, huku wakimtanguliza Mungu katika kufanya kazi, kusimamia maadili, kutenda haki, kutojihusisha na rushwa, kuwatumikia Watanzania bila kubagua dini, kabila wala vyama vyao.

“Kikubwa mkasimamie yale tuliyoyaahidi sisi wanaCCM, kwa sababu wakati tunazunguka tukiomba kura, yapo tuliyoyaahidi, hayo mkayatekeleze kwa nguvu zote.

“Na wala asitokee mtu yeyote wa kuwakwamisha kutekeleza hayo, ninyi ndio wakuu wa wilaya na ninyi watatu ndio wakuu wa mikoa. Mna mamlaka makubwa ya kuweka mahabusu mtu masaa 48 halafu kesho yake ukamwachia. Ila msiende kuonea watu, mkachape kazi.

“Imani tuliyoionyesha kwenu sisi viongozi wenu mkaionyeshe kwa Watanzania mnaowaongoza, mkashirikiane na viongozi mtakaowaongoza, wanasema umoja ni nguvu, utengano ni udhaifu.

“Nina uhakika mkisimama vizuri  kwa kuzingatia maadili mliyonayo, na bahati nzuri wengi mna uzoefu katika maeneo yenu. Mkawahamasishe Watanzania katika wilaya na mikoa yenu kufanya kazi. Watanzania wengi tumezoea kulalamika, tunataka tupewe, lakini hatufanyi kazi. Tukawasimamie kuchapa kazi,” alisema.

Aliwataka wakuu hao wa wilaya ambao pia ni wenyeviti wa kamati ya ulinzi na usalama, kukemea rushwa katika maeneo yao na kusimamia mapato ya Serikali.

“Huwa inatokea saa nyingine wakurugenzi kwa sababu kuna fedha nyingi tunapelekaga kule, wanadhani ni zao wakati ni za Serikali, mkawasimamie bila woga.

“Kupitia halmashauri zenu, mkahakikishe fedha hizo zinatumika kulingana na matakwa ya kanuni na sheria za nchi,” alisema Rais Magufuli.

Viewing all 45270 articles
Browse latest View live




Latest Images