Quantcast
Channel: MPEKUZI
Viewing all 45270 articles
Browse latest View live

Bungeni: Serikali Kuimarisha Miundombinu Kuboresha Utalii Nchini.

0
0

Serikali imejipanga kuimarisha miundombinu inayoelekea kwenye mbuga za wanyama na vituo vingine vya utalii nchini ili kuboresha utalii wa ndani na wa nje ya nchi kwa kujenga barabara ili kuwezesha watalii kufika kwa urahisi katika sehemu za vivutio vya kiutalii.

Akijibu swali la Mhe.Risala Said Kabongo Mbunge wa Viti Maalum (CHADEMA) lililouliza serikali ina mikakati gani kuboresha miundombinu ya barabara, malazi na viwanja vya ndege katika hifadhi, Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Ramo Makani amesema jitihada zimefanya na zinaendelea kufanywa ili kuboresha na kuimarisha barabara mbalimbali zinazoelekea katika hifadhi mbalimbali nchini kwa kiwango cha lami ili kuongeza wigo wa watalii kutembelea maeneo hayo kwa urahisi.

Amezitaja barabara ambazo zilizoko kwenye mpango wa kuziboreshwa ili kurahisisha watalii kuyafikia maeneo hayo kuwa ni barabara ya Sumbawanga-kasanga, barabara ya Kigoma kuelekea kusini hadi Kalya na Mwese.

“Sio tutaboresha barabara tu ila tunaviangalia pia viwanja vya ndege vinavyotumika kwa kuviimarisha na kuviboresha viwanja vya ndege vya Songwe,Kigoma na Mpanda ambavyo vitasaidia kufikika kwa urahisi maeneo ya vivutiio

“ Tunaendelea kuvutia wawekezaji binafsi kutoa huduma mbalimbali za watalii kama malazi na mpka sasa  tumetoa vibali 11 kwa wawekezaji kuwekeza katika malazi yaani Hoteli za kitalii katika Hifadhi za Ruaha,Mikumi,katavi na Mahale  na uwekezaji huo uko katika hatua za utekelezaji” Alisema Mhe. Ramo Makani.

Wizara kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) na Shirika la USAID inaandaa mikakati ya kuendeleza na kuutangaza utalii kwenye maeneo mbalimbali na kuboresha miundombimu ili kuwezesha watalii kufikia vivutio kiurahisi.

Waziri Wa Ujenzi, Uchukuzi Na Mawasiliano Profesa Mbarawa Amteua Bwana Masanja Kungu Kadogosa Kuwa Kaimu Mkurugenzi Mkuu Wa TRL

0
0

 WIZARA YA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI.

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa amemteua Bwana Masanja Kungu Kadogosa kuwa Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Reli Tanzania (TRL), ambako anakwenda kuchukua nafasi ya Mhandisi Elias Mshana ambaye anastaafu hivi karibuni.

Kabla ya Uteuzi huo Bwana Masanja Kadogosa alikuwa Mkurugenzi Idara ya Mikopo Benki ya Rasilimali Tanzania (TIB). Uteuzi huo unaanza mara moja.

Imetolewa na;
Kitengo cha Mawasiliano Serikalini.
02 Februari, 2016.

BAKWATA Waunga Mkono Uchaguzi wa Marudio Zanzibar

0
0

WAKATI Chama  cha wananchi CUF ambacho ni chama kikuu cha Upinzani visiwani Zanzibar kikiwa kimesusia uchaguzi wa marudio ambao unafanyika Marchi 20 ya mwaka huu,Baraza la Waislam  (BAKWATA)  limesema marudio ya  uchaguzi huo ndo njia ya kipee ya kurudisha amani visiwani humo..

Akizungumza na waandishi wa habari leo,Jijini Dar es Salaam, Sheikh Mkuu mkoani hapa,heikh alhadj Mussa Salum  amesema  Bakwata wanaunga mkono Tangazo la ZEC la kurudiwa kwa uchaguzi hu.
 
“Uchaguzi huu wa marudio  kwetu Bakwata tunaona ndio njia ya kipekee ya kukiweka kisiwa cha Zanzibar kuwa sehemu ya Amani na utulivu,natumia nafasi hii kuwaomba chama cha CUF kushiriki uchaguzi huu” Amesema Sheikh Salum.

Sheikh Salum ameongeza kwa kusema  kuwa hata kiongozi wa jumuiya ya Uamsho Visiwani Zanzibar, Sheikh Farid Hadi Ahmad amemwandikia barua na kumweleza kuwa kurudiwa kwa uchaguzi kutasaidia kurudisha Amani visiwani humo.
Katika hatua nyingine, Baraza hilo limeipongeza serikali ya awamu ya tano kwa jitihada mbalimbali inazofanya za kuimarisha nidhamu, kubana matumizi na kukuza uchumi.

"Pia tunaipongeza serikali ya awamu ya tano, inayoongozwa na Mh. John Magufuli, kutokana na hatua mbali mbali inazozichukua zenye lengo la kuimarisha nidhamu hasa kwa watumishi wa umma, hatua mabazo zimeanza kuleta tija kubwa ka taifa letu kama wote hivi leo tunavyoweza kushuhudia jinsi pato la serikali likongezeka mwezi hadi mwezi”, alisema Sheikh alhadj Mussa Salum  na kuongeza;

“Aidha tunaipongeza kwa dhamira yake ya kubana na kupunguza matumizi ya serikali, na badala yake kuelekeza fedha kwenye huduma za jamii na watanzania tumeshaanza kunufaika na huduma hizo kama vile suala la elimu bure."

 

Polisi Yapiga Marufuku maandamano ya vijana wa Chadema kwenda Ikulu Kesho

0
0

Jeshi la Polisi limetoa tamko kuhusu tangazo la Baraza la Vijana wa Chadema (BAVICHA) kuwa kesho wamepanga kufanya maandamano hadi Ikulu kwa lengo la kuishinikiza serikali kubadili msimamo wake kuhusu TBC kutorusha Live baadhi ya vikao vya Bunge.

Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Simon Siro amepiga marufuku maandamano hayo na kuwataka vijana hao kutumia njia mbadala za kupata ufumbuzi wa suala hilo badala ya maandamano.

Akitoa sababu za kuzuia kufanyika kwa maandamano hayo, Kamanda Sirro alisema kuwa hakuna taarifa  na pia hakuna uthibitisho kuwa maandamano hayo yatapokewa na Rais Magufuli.

Pia, Kamanda Sirro alieleza kuwa BAVICHA hawakuanisha barabara ambazo wanatarajia kutumia katika maandamano hayo.

“Siku hiyo sio nzuri sana kwa sababu ni siku ambayo watu wanakuwa kazini. Ni siku ambayo wengi watataka kutumia barabara hizo kwa ajili ya huduma za kijamii. Na kwa sababu kuna option nyingine ya kuweza kupata suluhu hiyo, nisema tu kwamba maandamano hayo yamepigwa marufuku,” alisema.

Jela miaka 5 kwa kusafirisha Wahamiaji Haramu

0
0

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Iringa imewahukumu kwenda jela miaka mitano au kulipa faini ya Sh milioni 1.5 kila mmoja, dereva Hansi Mwakyoma (28) na utingo wake, Alex Adam (32) baada ya kukamatwa na kukiri kusafirisha wahamiaji wasio na vibali 83 kutoka Ethiopia.

Wahamiaji hao wamehukumiwa kwenda jela miaka miwili au kulipa faini ya Sh milioni moja kila mmoja.

Kwa kutumia gari aina ya Scania lenye namba za usajili T478 DFE, mali ya Flora Mwambenja wa Mbeya, Januari 16, mwaka huu, dereva huyo na utingo wake, walikamatwa katika kijiji cha Ruaha Mbuyuni wilayani Kilolo Barabara Kuu ya Iringa - Mbeya, wakiwasafirisha watu hao kwenda Kyela mpakani mwa Tanzania na Malawi.

Akitoa hukumu hiyo juzi, Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mkoa wa Iringa, Andrew Scout alisema ameridhika na maelezo yaliyotolea na Wakili wa Serikali na vielelezo, likiwamo gari lililotumiwa na watuhumiwa hao kusafirisha watu hao kutoka Kongowe, Dar es Salaam kwenda Kyela mkoani Mbeya.

Baada ya kusoma hukumu hiyo, baadhi ya raia hao wa Ethiopia waliangua kilio mahakamani hapo na kusababisha watu waliokuwa karibu na jengo hilo, kusogea ili kujionea kulikoni.

Mkalimani wa wahamiaji hao, ambao hawazungumzi Kiingereza wala Kiswahili zaidi ya lugha ya kwao, Emmanuel Mtaltisili ambaye ni mtangazaji wa kituo cha redio ya Ebony FM cha mjini Iringa alisema; “walichokitarajia wahamiaji hao ni kupewa hukumu ya kurudishwa kwao baada ya kukiri kosa hilo.”

Awali akisoma maelezo ya kosa la watuhumiwa hao baada ya wote kukiri kosa mbele ya mahakama hiyo, Wakili wa Serikali kutoka Idara ya Uhamiaji, Godfrey Ngwijo alisema ilikuwa Januri 16, mwaka huu katika eneo la Ruaha Mbuyuni watuhumiwa hao walikamatwa wakiwa ndani ya gari hilo lenye bodi lililofunikwa, wakisafiri kutoka Kongowe kwenda Malawi kinyume cha Sheria ya Uhamiaji ya Mwaka 2002 iliyofanyiwa Marejeo mwaka 2015.

Alisema katika tarehe isiyojulikana, watuhumiwa 83 raia wa Ethiopia waliingia nchini kwa kutumia njia zisizo halali na kwenda Dar es Salaam, walikoanzia safari yao ya kwenda Kyela mkoani Mbeya ili waingie nchini Malawi.

TRA Yaendelea Kuikaba Koo StarTimes

0
0

Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), imesema Kampuni ya StarTimes inayouza ving’amuzi kwa ajili ya ‘chaneli’ mbalimbali za televisheni, ikiwamo Shirika la Utangazaji la Taifa (TBC) inafanya biashara ya simu kupitia mgongo wa mtu.

Hilo limebainika katika uchunguzi unaofanywa na TRA dhidi ya kampuni hiyo, kufuatia maboksi 294 yaliyokamatwa yakiwa na simu 2,744 na vifaa vyake ndani ya ghala lake mwezi uliopita.

Akizungumza jana, Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa Walipakodi, Richard Kayombo alisema uchunguzi unaoendelea kufanywa umebaini kuwa maboksi hayo yalikuwa ya StarTimes, tofauti na taarifa za nyaraka za mizigo zilivyokuwa zikieleza kuwa mizigo ni ya mtu mwingine.

“Tulifuatilia tukabaini hii biashara ambayo wanaifanya Startimes wanamtumia mtu mwingine kama sehemu ya kukwepa kodi, kwani nyaraka zilionyesha mzigo ni wa mtu mwingine, lakini katika kuchunguza tumebaini ni wa StarTimes,” alisema Kayombo.

Alisema wanaendelea na uchunguzi zaidi ili kujua kama biashara hiyo inayotumia jina la mtu imekuwa ikifanywa kwa muda gani, lakini pia wanaendelea kufanya utaratibu wa kampuni hiyo kulipa kodi ya mizigo hiyo.

“Bado tunafanya taratibu za namna ya kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria, ikiwa ni pamoja na kulipa kodi ambayo ilitakiwa ya Sh118 milioni,” alisema.

Mwenyekiti wa bodi ya StarTimes, Clement Mshana alipotafutwa kuzungumzia suala hilo alisema maswali hayo aulizwe Ofisa Mtendaji Mkuu wa kampuni hiyo, Lanfang Liao huku akisisitiza hana taarifa za kina kuhusu ripoti hiyo.

“Mwambie akufahamishe zaidi huyo ndiye mtendaji mkuu wa kampuni. Hata hivyo hiyo stori inayomkariri mtu wa TRA sijaisoma hivyo sina taarifa za kina juu ya alichoeleza TRA,” alisema.

Hata hivyo, alipoombwa namba yake ya simu hakuwa tayari kutoa, badala yake alituma ujumbe wa maneno uliosema kuwa “nimemwambia ofisa uhusiano atakupigia”.

Bodaboda Agonga Gari Na Kufariki Papo Hapo

0
0

DEREVA wa bodaboda, Colnery Mpande (18), mkazi wa Kiluvya Kwa Komba, amekufa baada ya pikipiki aliyokuwa akiiendesha kugonga gari kwa nyuma na yeye kuangukia barabarani na kukanyagwa kichwa na gari lingine.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani, Bonaventura Mushongi alisema pikipiki hiyo baada ya kuligonga gari hilo ilipoteza mwelekeo na kuanguka barabarani kisha kugongwa kwa kukanyagwa kichwa na kufa papo hapo.

Alisema tukio hilo ni la jana saa 10 alfajiri eneo la Mpakani, katika barabara ya Morogoro wilayani Kibaha.

Kamanda alisema gari aliloligonga kwa nyuma dereva huyo wa bodaboda lilisimama ghafla na halikuonesha ishara kwamba linakatisha kuingia kushoto.

Alisema Mpande alikuwa akiendesha pikipiki yenye namba za usajili MC 332 AXL aina ya Sanlg akitokea Kibaha kuelekea Kiluvya na aligonga gari lenye namba za usajili T 616 DCB aina ya Mitsubishi Canter lililokuwa likiendeshwa na Shaaban Ally kutoka Kibaha kwenda Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa Kamanda, Mpande alikanyangwa kichwa na lori la mizigo lenye tela na namba za usajili T 559 BFA/T 874 AQF likiendeshwa na Daniel Joseph aliyekuwa akitokea Dar es Salaam kwenda Mbeya.

Ahadi Ya Rais Mtaafu Kikwete Yaibuliwa Bungeni

0
0

Ahadi iliyotolewa na Rais wa Awamu ya Nne, Jakaya Kikwete, Januari 25, mwaka 2008, jana ilizua maswali bungeni baada ya Mbunge wa Dimani (CCM), Hafidhi Ali Tahil, kuhoji ni lini Serikali itaanza kuitekeleza.

Mbunge huyo alisema kushindwa kutekelezwa kwa ahadi hiyo ya Rais mstaafu hadi sasa, inatafsiriwa na baadhi ya watu kuwa alilenga kuwadanganya wananchi.

Katika swali lake la msingi, Tahil alitaka kujua ni lini Serikali itaanza kutekeleza ahadi ya ujenzi wa Kituo cha Afya cha Kichakapunda na ile ya kuunganisha umeme na maji kwenye Kijiji cha Jitimai hadi Skuli kama alivyoahidi Rais Kikwete kwenye moja ya ziara zake alizozifanya visiwani Zanzibar, 2008. 

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Luhwaga Mpina, akijibu swali hilo, alisema ahadi hiyo imechukua muda mrefu, lakini iko mbioni kutekelezwa kama ilivyoahidiwa.

Mpina alisema Serikali itatekeleza ahadi zote zilizotolewa, na tayari ofisi ya Wilaya ya Magharibi viliko vituo hivyo, imeshafanya mawasiliano na wizara zinazoshughulikia sekta ya afya na umeme ili hatua za utekelezaji zianze.

“Kwa sasa wananchi wa Kichakapunda wanapata huduma za afya kupitia vituo vya afya vya Kibondeni, Melitano na Fuoni, ambavyo vyote umbali wake kutoka Kichakapunda hauzidi kilomita tatu,” alisema Mpina.

Alisema kwa mujibu wa Sera ya Afya ya Zanzibar, masafa hayo yanakidhi haja ya upatikanaji wa huduma hizo.

Alisema mipango ya kujenga kituo hicho cha afya bado inafanyiwa kazi wakati huduma ya umeme imekwishafika eneo la Hado.

Waziri Wa Mambo Ya Nje Augustine Mahiga Ala Kiapo Bungeni Akiwa Mpweke

0
0

Kiapo cha uaminifu cha Waziri wa Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Kimataifa, Kikanda na Kimataifa, Dk Augustine Mahiga jana, kilikuwa sawa na viapo vingine, lakini alikosa vionjo kama ilivyokuwa kwa wenzake.

Mwanzoni mwa mkutano wa pili wa Bunge la 11, mawaziri na naibu mawaziri walioteuliwa na Rais John Magufuli walikula kiapo cha utii kwa Bunge ili kutimiza majukumu yao.

Katika viapo hivyo kulikuwa na mbwembwe nyingi kutoka kwa wabunge, hasa wanawake ambao kila lilipoitwa jina la mtu walipiga kelele na kumsindikiza hadi mbele alipokuwa akiwaapishia Spika. 

Hali ilikuwa tofauti jana, wakati Dk Mahiga alipoitwa kwa ajili ya kura kiapo maana hakukuwa na mbwembwe wala vigelegele kutoka kwa wabunge na pia aliingia akiwa peke yake na mpambe wa Bunge aliyekuwa anamuongoza.

Haikujulikana ni wapi walikokuwa wabunge wa CCM ili wamshangilie waziri, jambo lililoonyesha upweke kwa upande wake, ikizingatiwa hata Waziri Mkuu hakuwa kwenye kiti chake na kiongozi wa upinzani pia hakuwapo ambao utaratibu huwapa nafasi ya kuwakabirisha wabunge wapya. 

Sakata La Mauaji Ya Diwani Wa CUF Lachukua Sura Mpya

0
0

Mauaji ya kikatili ya Diwani wa Kata ya Kimwani, Wilaya ya Muleba mkoani Kagera, Sylvester Muliga (CUF), yameanza kuibua mambo mazito huku ikielezwa kuwa Ijumaa alikuwa awasilishe hoja kwenye Baraza la Madiwani kuhusu masuala ya ardhi.

Muliga ambaye alifia Hospitali ya Kagondo alikopelekwa kwa matibabu baada ya kukatwa mapanga Jumapili usiku, imeelezwa kuwa katika kikao hicho ilikuwa aombe kuundwa kwa kamati ya kuchunguza uhalali wa maeneo makubwa ya ardhi yanayomilikiwa na watu wachache.

Kwa mujibu wa mjumbe wa Kamati ya Uchumi na Mazingira ambaye pia ni Diwani wa Kata ya Kasharunga, Khalid Swalehe, hoja hiyo ilikuwa iwasilishwe na Muliga na ilikuwa inaungwa mkono na madiwani wa kata zote zilizo na migogoro ya ardhi.

Baada ya taarifa za kufariki dunia kwa diwani huyo, wananchi walivamia nyumba nane za watuhumiwa wanaodaiwa kutekeleza mauaji hayo na kuziteketeza kwa moto.

Pia, walichoma moto mashine mbili za kusaga na kuharibu gari la mmoja wa wagombea wa udiwani katika Uchaguzi Mkuu uliopita.

Kwa mujibu wa Mwenyekiti wa Kijiji cha Kyota, Daudi Kiruma, wananchi wamehusisha mauaji hayo na mambo ya siasa.

“Kinachoonekana hapa baadhi ya watu wanataka kupotosha ajenda ili wahusika wa mauaji wapate nafasi ya kutoroka,” alisema Kiruma.

Hata hivyo, Kiruma alisema hana uhakika kama mtuhumiwa anayedaiwa alikuwa mgombea amekamatwa, kwa sababu haonekani.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kagera, Augustine Ollomi, jana alisema wanamshikilia mtuhumiwa mwingine ambaye anafanya idadi ya walikomatwa kuhusiana na mauaji hayo kufikia watatu mpaka sasa.

Kamanda Ollomi aliwataka wananchi wasijadili mauaji hayo kwa hisia za kisiasa bali waviachie vyombo vya dola vifanye kazi yake.

Kaya 50 karibu na ghorofa 16 eneo la Indira Ghandi zapewa siku 3 kupisha zoezi la Kulibomoa

0
0

Zaidi ya kaya 50 zinazoishi kuzunguka jengo la ghorofa 16 lililopo mtaa wa Indira Gadhi katikati ya jiji ambalo linatakiwa kubomolewa zimepewa siku tatu ziwe zimeondoka kwa muda ili kupisha zoezi hilo ambalo litachukuwa miezi mitatu hadi kukamilika.
 
Mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam Saidi Mecky Sadiki ametoa agizo hilo mara baada ya kutembelea eneo hilo ambapo amesema lengo la wao kutakiwa kuondoka ni kunusuru maisha yao na kwamba baadhi ya barabara nazo zitafungwa huku akielezea sababu zilizochelewesha zoezi hilo la ubomoaji kuanza.

Baadhi ya wananchi wanaotakiwa kupisha zoezi hilo wamepongeza hatua hiyo na kudai kuwa walikuwa wanaishi kwa mashaka kwa kipindi chote hicho na wengine wakihoji utaratibu wa gharama za kuhama kwa madai kuwa hawana uwezo wa kwenda kupangisha hoteli miezi yote hiyo.

Akizungumzia zoezi hilo mkurugenzi wa manispaa ya Ilala Bw Isaya Mngulumi amesema baada ya kikao cha ulinzi na usalama cha mkoa kumalizika watatoa taarifa ya maandishi kwa wakazi hao ya kuhama

Uamuzi wa kubomoa jengo hilo umechukuwa zaidi ya miaka mitatu tangu lilipobainika kuwa limejengwa chini ya kiwango na halikuzingatia vibali vya ujenzi kwani lilipewa kibali cha kujenga ghorofa 10 badala yake wakajenga ghorofa 16.

Bei ya Mafuta Yashuka Tena

0
0

Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (Ewura), imetangaza bei kikomo ya mafuta, ambapo bei ya dizeli imeshuka kutoka Sh. 1,747 hadi Sh 1,600, likiwa ni punguzo la Sh. 147 kwa lita.

Kadhalika, bei ya mafuta ya petroli imeshuka kwa Sh. 55, hivyo kufanya mafuta hayo kuanzia leo kuuzwa kwa bei isiyozidi Sh. 1,842 kutoka Sh. 1,898 kwa lita kama kilivyokuwa ikiuzwa mwezi uliopita.

Taarifa iliyotolewa jana jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Mkuu wa Ewura, Felix Ngamlagosi, ilieleza kuwa, kupungua kwa bei ya mafuta kwenye soko la ndani  kwa kiasi kikubwa kumetokana na kushuka kwa bei ya nishati hiyo katika soko la dunia na pia kushuka kwa gharama za usafarishaji na bidhaa za mafuta hayo kuja nchini.

“Hakukuwa na mafuta ya taa yaliyoingizwa nchini Januari mwaka huu, hivyo Februari bei ya bidhaa hii itaendelea kuwa kama ilivyokuwa kwa Januari ambayo ni Sh. 1,699 kwa lita kwa soko la Dar es Salaam,” alisema.

Ngamlagosi alisema kushuka kwa namna hiyo kulitokea Machi, mwaka jana, lita moja ya mafuta ya dizeli ilishuka hadi kufikia Sh. 145 na dizeli kuzwa kwa Sh. 1,563 kwa lita.

Mkurugenzi huyo wa Ewura aliwaomba wananchi kupuuza uvumi unaoenezwa kuwa mamlka hiyo haipendi kushusha bei za mafuta kwa kuwa kushuka kwake kutaadhiri mapato.

Alisema tozo ya Ewura inatokana na kiasi cha lita za mafuta kinachouzwa na si kupanda kwa bei.

Aidha, amewakumbusha wamiliki wa vituo vyote vya mafuta kubandika bei za bidhaa za mafuta katika mabango yanayoonekana bayana, yakionyesha bei ya mafuta, punguzo, vivutio vya biashara na promosheni zinazotolewa na kituo husika.

Spika Wa Bunge Job Ndugai Akubali Kuzifumua Kamati Za Bunge.....Zitto Kabwe Kurudishwa PAC, James Mbatia Kamati Ya Bajeti

0
0

Baada ya malalamiko ya wabunge wa upinzani juu ya wajumbe wa kamati za kudumu za Bunge, Spika wa Bunge, Job Ndugai, anatarajia kuzipangua kamati hizo.

Taarifa za uhakika toka Bungeni mjini Dodoma zinasema, licha ya kuwapo kwa baadhi ya wajumbe walioomba kuhamishwa kwenye kamati walizopangiwa awali, kumekuwapo na mazungumzo kati ya Kambi ya Upinzani Bungeni na kiti ofisi ya Spika juu ya suala hilo.

Inaelezwa kati ya wajumbe watakaohamishwa kutoka kwenye kamati zao za awali ni Mbunge wa Kigoma Mjini (ACT-Wazalendo), Zitto Kabwe aliyekuwa kwenye Kamati ya Maendeleo ya Jamii na sasa atapelekwa  Hesabu za Serikali (PAC).

Naye Mbatia aliyekuwa mjumbe wa Kamati ya Miundombinu, sasa atapelekwa kwenye Kamati ya Bajeti aliyokuwa akitumikia kwenye Bunge la 10.

Spika wa Bunge, alipotafutwa ili kuzungumzia suala hilo kupatikana.

Juzi Mnadhimu wa Kambi ya Upinzani Bunge, Tundu Lissu, alisema wanafikiria kumpeleka Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe, kwenye kamati ya PAC ili awe mwenyekiti wao.

“Wasipokubali (kubadilisha wajumbe) hatutakubali ungozi tutaacha, mimi mwenyewe sheria ndogo siendi, huko ni kupoteza muda kwa sababu hakuna kamati ya ovyo vile, nitaenda sheria na katiba na kushiriki mijadala, kura tu ndiyo sintopiga, hoja yoyote ya kisheria ikiibuka bungeni nitaibuka na watashangaa,” alisema Lissu.

Serikali Iongeze Nguvu Kuusambaratisha Mtandao wa Majangili

0
0
 (Katibu Mkuu wa Maliasili na Utalii Meja Jenerali Gaudence Milanzi)

Wiki iliyopita helikopta ya doria iliyokuwa ikifanya kazi kwenye Pori la Akiba la Maswa mkoani Simiyu ilishambuliwa na majangili na kumuua kwa risasi rubani wake, Rodgers Gower.

Tukio hilo limetokea wakati Serikali ikiongeza nguvu kwenye vita dhidi ya majangili ambayo yanatishia kutoweka kwa baadhi ya wanyama kama tembo, ambao ndovu zake ni nyara zenye thamani kubwa duniani.

Bila shaka tukio la kuuawa kwa rubani wa helikopta hiyo limeanza kutuaminisha kwamba shughuli hiyo ya ujangili sasa inafanywa kijeshi na kwa kutumia wataalamu.

Kwa maneno mengine, tukio hilo linatuma ishara kwamba vita dhidi ya ujangili si lelemama kwa kuwa sasa haifanywi na watu wenye njaa tu ya fedha, bali watu wenye utaalamu wa hali ya juu na wanaoweza kupambana na yeyote anayejaribu kuwaharibia biashara yao.

Na kwa maneno mengine ni kwamba juhudi zinazofanyika hadi sasa ni za kupambana na dalili tu na si mzizi wenyewe wa ujangili, ambao ni mtandao unaohusisha watu wengi wa sehemu tofauti; kuanzia wanakijiji wa vijiji vinavyozunguka mbuga na hifadhi zetu, watendaji wizarani, polisi, hadi wanasiasa.

Ndiyo maana tembo wanauawa na pembe zao kuhifadhiwa hadi mzigo unapotosha na kusafirishwa kutoka mbugani au kwenye hifadhi hadi Uwanja wa Ndege au bandarini na pengine hata kufanikiwa kupitishwa, bila ya wasafirishaji au wauaji kung’amuliwa.

Hiyo ina maana kwamba si wanakijiji wanaostukia harakati hizo za kukusanya pembe za ndovu, wala askari wa Idara ya Wanyamapori, wala polisi wanaokagua mizigo wanayoishuku, wala maofisa walio bandarini au uwanja wa ndege ambao wanafanikiwa kukamata mizigo hiyo hadi inatoka nje ya mipaka.

Huu ni mtandao mkubwa na wenye nguvu ambao unahitaji juhudi za ziada kuusambaratisha.

Kwa hiyo, vita dhidi ya ujangili haitakiwi iwe ya maneno mepesi, bali iwe inayoonyesha ugumu uliopo na ni jinsi gani umma unavyoweza kushiriki kupambana nao.

Vita hiyo inahitaji mkakati mkali ambao malengo yake yawe ni kuungamiza mtandao wa ujangili na si kupunguza vitendo hivyo kwa sababu kama majangili wameanza kupata ujasiri wa kushambulia kwa silaha kali watu wanaojaribu kuwadhibiti, ni dhahiri kuwa wameingia vitani na hawataki mchezo tena.

Ni wakati mwafaka sasa kwa Serikali kuchukulia tukio la kuuawa kwa rubani huyo kuwa mwanzo wa kuung’amua mtandao wa majangili na kukusanya taarifa nyingi kabla ya kuanza vita ya kupambana na uovu huo. Kukiwa na nia ya dhati, ujangili utaangamizwa.

Vyama Vitano Kushiriki Uchaguzi Wa Marudio Zanzibar

0
0

Vyama vitano vya siasa vitashiriki katika uchaguzi wa marudio wa Zanzibar, utakaofanyika Machi 20 mwaka huu, uliotangazwa na Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC). Vyama hivyo ni Chama Cha Mapinduzi (CCM), ADC, CCK, TLP na SAU.

Hatua hiyo inatokana na vyama vitatu vya siasa Zanzibar vya CCK, SAU na TLP, kutangaza kuwa wagombea wake, watashiriki katika uchaguzi huo wa Machi 20. Taarifa ya viongozi wa vyama vya CCK, SAU na TLP, iliyosomwa kwa pamoja katika Ukumbi wa Culture eneo la Mji Mkongwe  jana, ilisema wagombea wa vyama hivyo vitatu, watashiriki uchaguzi huo.

Taarifa hiyo ilieleza kuwa Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25, mwaka jana, ulifutwa baada ya kujitokeza kwa kasoro mbalimbali, zilizoonesha wazi kwamba hauwezi tena kuwa huru na haki. 

Wagombea wa vyama hivyo vya siasa, waliotangaza kushiriki katika uchaguzi huo ni Ali Khatib kutoka CCK, Issa Mohamed Zonga kutoka SAU na Hafidh Hassan Simai kutoka TLP.

Mgombea wa CCK, Ali Khatib Ali alisema kwamba tayari wamejipanga vizuri kwa ajili ya uchaguzi huo na kuwataka wanachama na wafuasi wake na wananchi, kuitumia fursa hiyo ya kidemokrasia kuchagua viongozi watakaoongoza nchi. 

“Tangazo la Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) limetutaka kurudia uchaguzi kwa sababu ule wa awali umefutwa kwa hivyo hatuna sababu ya kususia uchaguzi huo na tunachofanya kwa sasa ni kuwataka wanachama wetu na wafuasi kujitayarisha kwa uchaguzi wa marudio,” alisema Ali.

Jumapili iliyopita, Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein alisema chama hicho kipo tayari kwa uchaguzi wa marudio Machi 20 kwa lengo la kuhakikisha kinashika dola. 

Akihutubia mamia ya wanachama wao katika viwanja vya Ofisi Kuu ya CCM Kisiwandui wakati wa kuzindua maadhimisho ya miaka 39 ya CCM, Dk Shein alisema maamuzi ya kurudiwa kwa Uchaguzi Mkuu, yamefanywa na ZEC ambayo ndiyo chombo halali kwa mujibu wa Katiba cha kushughulikia masuala yote ya uchaguzi nchini.

Aliwataka wanachama na wafuasi wao kujipanga vizuri na kushiriki uchaguzi huo kikamilifu, kwani kwa mujibu wa Katiba ya CCM ni kushinda chaguzi zote zinazofanyika nchini ili kushika dola na kuwatumikia wananchi.

“Hayo ndiyo maamuzi ya chama chetu tuliyokubaliana kushiriki Uchaguzi Mkuu wa marudio baada ya kufutwa kwa ule wa Oktoba 25 mwaka jana kwa hivyo wanachama na wafuasi jitayarisheni kushiriki kikamilifu kwa ajili ya kushika dola,” alisema Dk Shein.

AUDIO: Mnyukano wa Halima Mdee na Dk. Mwakyembe Bungeni Jana Febr 2 Kuhusu Sakata La Mabehewa Mabovu

0
0

Waziri wa Sheria na Katiba, Dk. Harrison Mwakyembe na Mbunge wa jimbo la Kawe, Halima Mdee (Chadema), jana waliingia kwenye mvutano mkali huku wakitunishiana misuli ya sheria kuhusu kashfa ya ununuzi wa mabehewa 274 yanayodaiwa kuwa mabovu. Ununuzi huo uliofanywa wakati Dk. Mwakyembe alipokuwa Waziri wa Uchukuzi.

Mdee aliibua tena suala la kashfa ya ununuzi wa mabehewa hayo 274 akisisitiza kuwa ni mabovu, wakati alipopata nafasi ya kuchangia katika Mpango wa Maendeleo wa mwaka 2011/- 2015/16 ambapo aligusia ahadi ya serikali ya kukarabati reli ya kati  ambayo alidai haijatekelezwa ipasavyo.

Dk. Mwakyembe alikanusha taarifa ya kuwepo kwa mabehewa mabovu kati ya mabehewa hayo 274 yaliyonunuliwa wakati akiwa Waziri wa Uchukuzi.

 “Leo nikimwambia Halima aniletee mabehewa ambayo hayafanyi kazi atashindwa kunionesha,” alisema  Mwakembe

Waziri huyo alieleza kuwa mkataba wa ununuzi wa mabehewa hayo ulitoa mwanya wa kufanya ukarabati au marekebisho katika bidhaa husika ndani ya muda fulani, kipengele kinachojulikana kama ‘defect liability period’. 

Hivyo, alitumia kipengele hicho kufanyia marekebisho mabehewa hayo ambayo alikiri hayakuwa mazuri yalipowasilishwa.

“Mabehewa yote yanafanya kazi kwa sababu yalipoletwa ni mimi mwenyewe nilisema kuna mabehewa ambayo sio mazuri. Nikaunda uchunguzi, kwa sababu tulikuwa na haki chini ya mkataba (defects liability period), ilikuwa ndani ya mwaka mmoja, wakaja wale walioutuuzia mabehewa wakayatengeneza. Sasa yako wapi hayo mabovu?” alieleza Mwakyembe.

Juzi, Mwakyembe alieleza kuwa yuko tayari kujiuzulu ubunge wake kama itabainika kuwa madai ya kashfa hiyo ni ya kweli.

 Hata hivyo, baadhi ya wabunge wa upinzani walitaka ripoti ya uchunguzi wa ununuzi wa mabehewa hayo iwasilishwe bungeni huku wakisisitiza kuwa kulikuwa na ukiukwaji wa sheria ya ununuzi iliyopelekea ununuzi wa mabehewa mabovu.

===> Sikiliza Hapo Mnyukano ulivyokuwa Bungeni

Dr. Slaa Ajibu Mapigo....Akanusha Nyumba Yake Kupigwa Mnada Kisa Mkopo Aliochukua Mkewe Na Kumpa Mwanaume Mwingine

0
0

Katibu Mkuu wa Zamani wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk. Wilbroad Slaa ametoa majibu kuhusu taarifa zinazoandikwa kwenye baadhi ya magazeti nchini pamoja na mitandao kuwa nyumba yake iliyoko Mbezi jijini Dar es Salaam inauzwa baada ya kushindwa kulipa mkopo wa Benki ikidaiwa kuwa mkewe aliuchukua na kumpa mwanaume mwingine.

Taarifa hizo zilieleza kuwa Mke wa Dk. Slaa, Josephine alichukua mkopo wa shilingi milioni 300 katika moja kati mabenki nchini na kushindwa kuirudisha fedha hiyo.

Dk. Slaa ambaye yuko nchini Canada akijiendeleza kimasomo, amekanusha taarifa hizo na kueleleza kuwa yeye na mkewe Josephine hawajawahi kuchukua mkopo katika benki yoyote nchini.

“Nataka nikuambie na uwajulishe Watanzania kwamba wala si mimi Dk. Slaa wala mke wangu, Josephine kwa wakati wowote ule hatujawahi kuchukua mkopo benki,” Dk. Slaa aliliambia gazeti la Mtanzania kwa njia ya simu.

“Tangu nitoke Bungeni sijawahi kuchukua hata senti moja benki, achilia mbali propaganda ya shilingi milioni 300.

" Hivyo, ni vizuri waliokupa taarifa wakupe undani ni benki ipi nilikopa au Josephine alikopa na ni shilingi ngapi na kwa nyaraka zipi. 

"Na ni vema ukafuatilia benki husika pia kama walikuwambia ni benki gani,” Mwanasiasa huyo mkongwe alieleza.

Dk. Slaa ambaye alitangaza mwaka jana kustaafu siasa, alisema kuwa anapanga kuchukua hatua za kisheria dhidi ya wote walioandika habari hizo.

Mkoa Mpya wa Songwe na Wilaya Mpya Zaanishwa

0
0


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.John Pombe Joseph Magufuli ameidhinisha kuanzishwa kwa mkoa mpya wa Songwe na wilaya nyingine mpya nchini.

Akitoa tamko hilo kwa niaba ya Rais Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa(TAMISEMI) Mhe George Simbachawene amesema kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 imempa Mamlaka Rais ya kugawa Nchi kwa kadri ambavyo atakapoona inafaa.

Mhe George Simachawene amesema kutokana na mamlaka hayo aliyopewa Rais jumla ya Wilaya sita na Mkoa mmoja wa Songwe umeanzishwa kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 na Mkoa mpya wa Songwe umeanzishwa kutoka Mkoa wa Mbeya.

Amezitaja Wilaya mpya zilizoanzishwa kuwa ni Wilaya ya Songwe Mkoa wa Songwe,Wilaya ya Ubungo Mkoa wa Dar es salaam, Wilaya ya Kibiti Mkoa wa Pwani, Wilaya ya Kigamboni Dar es salaam, Wilaya ya Mlanyi Mkoa wa Morogoro na Wilaya ya Tanganyika Mkoa wa Katavi

“ Nichukue fursa hii kuwaagiza Wakuu wa Mikoa wote ambao Wilaya mpya zimeanzishwa kufanya maandalizi rasmi ili Mkoa na Wilaya hizo ziweze kuanza kufanya kazi,aidha mkazo uwekwe kwenye upatikanaji wa Ofisi na huduma zote muhimu kupatikana kwa urahisi katika Mkoa naWilaya hizo mpya” Alisema Mhe Simbachawene.

Polisi Kudhibiti Uporaji Wa Fedha Kwenye Mabenk

0
0
(Na Raymond Mushumbusi-MAELEZO)
Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kupitia Jeshi la Polisi imejipanga kudhibiti uhalifu unaofanywa na na baadhi watu kwa kupora fedha za wafanyabiashara au watu binafsi kwa kutumia usafiri wa Pikipiki maarufu kama bodaboda.
 
Akijibu swali la Mhe. Oscar Rwegasira Mukasa Mbunge wa Biharamulo Magharibi (CCM) lililouliza ni zipi takwimu sahihi za matukio ya ujambazi yanayohusiana na uporajiwa fedha,Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mhe. Hamad Yussuf Massauni amesema matukio ya ujambazi yanayohusisha uporaji wa fedha kwa kipindi cha kuanzia mwaka 2013 hadi 2015 kama takwimu zinavyosema , kwa mwaka 2013 matukio 1.266, mwaka 2104 matukio 1,127 na mwaka 2015 yalikuwa 931.
 
” Jeshi la polisi limechukua hatua kwa kufanya kazi karibu na mabenki nchini ili kubaini kama kuna wafanyakazi wa mabenki wanashirikia na majambazi kufanya uporaji huo na watakaobainika tutawachukulia hatua kali za kisheria ikiwa ni pamoja na kuwafikisha mahakamani watakaokamatwa”
 
“ Napenda kuwaomba wananchi kutupa ushirikiano na hasa kwa wafanyabiashara wanaochukua fedha nyingi ili tuweze kuwapatia ulinzi ili kupunguza, ama kuondoa kabisa vitendo hivi vya uporaji wa fedha vilivyokothiri nchini kwa sasa” Alisema Mhe Massauni.
 
Aidha amewaomba waheshimiwa Wabunge kutoa elimu kwa wananchi wao kuhusu maswala ya ulinzi na usalama ili kupunguza vitendo vya uhalifu hasa uporaji wa fedha kwa wafanyabiashara kwa kutoa taarifa kwa Jeshi la Polisi wakiona tukio lolote linalopangwa kwa ajili ya kupora fedha.
 
Serikali kupitia Jeshi la Polisi linafanya ukaguzi wa pikipiki zote nchini ili kubaini uhalali wake na uhalali wa wamiliki wake ili kuweza kubaini pikipiki na wamiliki wanaohusika na vitendo vya uporaji wa fedha vinavyoshamiri siku hadi siku

Mke wa Rais Mama Janeth Magufuli Atembelea Kambi Ya Wazee Wasiojiweza Na Walemavu Ya Nunge........Awaomba Wadau Mbalimbali Kujitokeza Kuwasaidia

0
0
Mke wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Mama Janeth Magufuli ameziomba na kuzihamasisha taasisi za Serikali na zisizo za Serikali kushirikiana na Serikali kutatua changamoto mbalimbali zinazozikabili Kituo cha Makazi ya Wazee na Watu Walemavu Wasiojiweza kijulikanacho kwa jina la Nunge,viwemo vingine.

Aidha alisema vituo hivyo  jumla vipo 17, katika maeneo  mbalimbali nchini.

Kauli hiyo imetolewa leo na Mama Magufuli wakati alipotembelea makazi hayo yaliyoko Kigamboni eneo la Vijibweni jijini Dares Salaam, ambapo  alisema changamoto wanazokabiliana nazo  amezisikia na na aliwaahidi kuwa  atashirikiana na wadau wote kuzitafutia majibu yake.

Mama Magufuli alizitaja baadhi ya  changamoto hizo,  kuwa ni  uchakavu wa miundombinu, uhaba wa rasilimali fedha na watu, pamoja na maslahi duni ya watoa huduma, upungufu wa vitendea kazi na huduma za jamii, pamoja na uvamizi wa eneo la kituo.

Aidha Mama Magufuli alimwomba Mkuu wa Wilaya ya Temeke, Sophia Mjema kulishughulikia taizo la uvamizi wa eneo hilo na kulitafutia ufumbuzi.

“ Natumaini  zawadi  tuliyoileta ni ndogo na haiwezi kumaliza matatizo yote mliyonayo. Lakini ni matumaini  yangu kuwa zawadi hii inaweza kuwa chachu ya kuhamasisha hamasa ya watu na vikundi vingine kujitoa kusaidia watu wasiojiweza.  

"Ni imani  yangu kuwa endapo watu wote tutajitoa  kwa dhati tutaweza kuwahudumia wazee na watu  wasiojiweza na hivyo kuwapunguzia  makali ya maisha . Tukumbuke ‘kutoa ni moyo na si utajiri’ na kwamba “sisi sote ni wazee na walemavu watarajiwa”.

Aliongeza kwamba ni  dhahiri kuwa Serikali ina wajibu mkubwa katika kuhudumia wazee na watu wasiojiweza. Hata hivyo Serikali pekee haiwezi kumaliza matatizo yote yanayowakabili na wazee na watu wasiojiweza.

 Hivyo basi, sote kwa pamoja tunao wajibu wa kusaidia nguvu za  Serikali  katika kuwahudumia watu hao.

“Na kwa kutambua hilo , mimi  na wenzangu  niliombatana nao  tumeamua kutoa zawadi yetu ndogo kwenu. Zawadi  hiyo inajumuisha vitu vifuatavyo mchele kilo 3000, unga kilo 3000 na maharage kilo 1200. Kulingana na idadi yenu niliyopewa kila mmoja atapewa kilo 25 za mchele, kilo 25 za unga na kilo 10 za maharage.

“Nawaombeni mniruhusu pia kuchukua nafasi hii kuwasilisha kwenu salamu nyingi kutoka kwa Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

"Ameniomba niwaarifu kuwa yupo pamoja nayi na kwamba Serikali itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali katika kuhakikisha wazee na watu wasiojiweza wanapata huduma zote muhimu kwa kadri ya uwezo wake,” alisisitiza  Mama Magufuli.

Mama Magufuli aliongeza kwamba wazee na watu wasiojiweza wanahitaji upendo, kuthaminiwa nakusaidiwa.

Hivyo kipimo kimojawapo cha kupima jamii iliyostaarabika na inayoheshimu misingi ya utu ni kuangalia namna inavyo wathamini wazee na watu wasiojiweza.

Aliupongeza uongozi na watumishi wote wa kituo hicho na vituo vingine nchini kwa kazi kubwa wanayoifanya licha ya kukabiliwa na changamoto kadhaa.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Temeke , Sophia Mjema alimtaka kila mwananchi kutambua kwamba bila wazee hakuna tutakachoweza kufanya hivyo ni muhimu kuwa enzi na kuwasaidia wazee walioko majumbani na mitaani.

“Tuwaenzi wazee na kuwasaidia pia hata wale walioko mitaani tuwashauri warudi majumbani ili Serikali iweze kuwaorozesha kwa kuwa si vizuri kukaa barabarani, Serikali ya Awamu  ya Tano ya Rais Magufuli itahakikisha inawajali wazee,” alisema.

 Akizungumzia kuhusu watoto wa mitaani alisemani wajibu wa wazazi kuhakikisha wanawalea watoto wao vizuri ili wasikilimbile mitaani kwa kuwa watoto ni taifa la kesho.

Naye Mwenyekiti wa wazee wa makazi hayo, Anthony Kikongoti alimshukuru Mama  Magufuli kwa niaba ya wenzake, kwa kuanza ziara yake ya kwanza ya kutembelea kituo hicho ,ambapo alimwomba apeleke salamu zao kwa baba  yao ambaye ni Rais Magufuli kuwa wanasema asante.

“Huu ni mwaka wa wanyonge dini zote tumwombee kwa pamoja ili aweze kuendelea kupunguza makali ya maisha,” alisema.

 Afisa Mfawidhi wa kituo hicho, Ojuku Mgedzi alisema wanahitaji bajeti ya kutosha ya kuendesha shughuli mbalimbali, watumishi 42 , wakiwemo walinzi, kwa kuwa waliopo  sasa ni 29 na  hawatoshi.

Alisema eneo hilo lina hekari 50.8 na nusu ya eneo hilo limevamiwa.

Mgedzi alisema kituo hicho kina idadi yawakazi 112, ambapo alimkabidhi Mama  Magufuli orodha ya idadi ya watu hao.

Mke wa Rais Mama Janeth Magufuli akisikiliza taarifa kutoka kwa Bw. Ojuku Mgedzi, Mkuu wa  Kituo cha Makazi ya Wazee na Watu Walemavu cha Nunge, Kigamboni, jijini Dar es salaam alikotembelea na kusikiliza mahitaji yao pamoja na kutoa msaada wa mchele kilo 3000, Unga kilo 3000 na Maharage Kilo 1200 ikiwa msaada wake kwa wazee na walemavu hao.
Mke wa Rais Mama Janeth Magufuli akipokea taarifa kutoka kwa Bw. Ojuku Mgedzi, Mkuu wa  Kituo cha Makazi ya Wazee na Watu Walemavu cha Nunge, Kigamboni, jijini Dar es salaam alikotembelea na kusikiliza mahitaji yao pamoja na kutoa msaada wa mchele kilo 3000, Unga kilo 3000 na Maharage Kilo 1200 ikiwa msaada wake kwa wazee na walemavu hao.
Mke wa Rais Mama Janeth Magufuli akioneshwa maeneo mbalimbali  na Bw. Ojuku Mgedzi, Mkuu wa  Kituo cha Makazi ya Wazee na Watu Walemavu cha Nunge, Kigamboni, jijini Dar es salaam alikotembelea na kusikiliza mahitaji yao pamoja na kutoa msaada wa mchele kilo 3000, Unga kilo 3000 na Maharage Kilo 1200 ikiwa msaada wake kwa wazee na walemavu hao.
Mke wa Rais Mama Janeth Magufuli akisalimiana na wagonjwa waliofika kupata huduma katika zahanati ya  Kituo cha Makazi ya Wazee na Watu Walemavu cha Nunge,  Kigamboni, jijini Dar es salaam alikotembelea na kusikiliza mahitaji yao pamoja na kutoa msaada wa mchele kilo 3000, Unga kilo 3000 na Maharage Kilo 1200 ikiwa msaada wake kwa wazee na walemavu hao.
Mke wa Rais Mama Janeth Magufuli akitembelea chumba cha kujifungulia cha zahanati ya  Kituo cha Makazi ya Wazee na Watu Walemavu cha Nunge, Kigamboni, jijini Dar es salaam alikotembelea na kusikiliza mahitaji yao pamoja na kutoa msaada wa mchele kilo 3000, Unga kilo 3000 na Maharage Kilo 1200 ikiwa msaada wake kwa wazee na walemavu hao.
Mke wa Rais Mama Janeth Magufuli akisalimiana kwa furaha na wakaazi wa  Kituo cha Makazi ya Wazee na Watu Walemavu cha Nunge, Kigambo ni, jijini Dar es salaam alikotembelea na kusikiliza mahitaji yao pamoja na kutoa msaada wa mchele kilo 3000, Unga kilo 3000 na Maharage Kilo 1200 ikiwa msaada wake kwa wazee na walemavu hao.
Mkuu wa wilaya ya Temeke Mhe Sophia Mjema akimkaribisha Mke wa Rais Mama Janeth Magufuli kuhutubia wakaazi wa  Kituo cha Makazi ya Wazee na Watu Walemavu cha Nunge, Kigambo ni, jijini Dar es salaam alikotembelea na kusikiliza mahitaji yao pamoja na kutoa msaada wa mchele kilo 3000, Unga kilo 3000 na Maharage Kilo 1200 ikiwa msaada wake kwa wazee na walemavu hao.
Mke wa Rais Mama Janeth Magufuli akihutubia wakaazi wa  Kituo cha Makazi ya Wazee na Watu Walemavu cha Nunge, Kigambo ni, jijini Dar es salaam alikotembelea na kusikiliza mahitaji yao pamoja na kutoa msaada wa mchele kilo 3000, Unga kilo 3000 na Maharage Kilo 1200 ikiwa msaada wake kwa wazee na walemavu hao.
Viewing all 45270 articles
Browse latest View live




Latest Images