Majid Abdulkarim
Uongozi wa Jiji la Dodoma umetakiwa kuandaa mpango mkakati wa kutangaza maeneo ya biashara na uwekezaji hususani miradi inayoendelea kujengwa ya soko kuu na kituo kikuu cha Mabasi jijini Dodoma.
Hayo yamebainishwa jana na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Selemani Jafo katika ziara yake ya kukagua miradi ya maendeleo katika Jiji la Dodoma.
“Sasa hivi andaeni utaratibu maalum wa kutangaza miradi hii ambayo itakamilika hivi karibuni, kama ni Kampuni itakayosimamia na kuendesha miradi hii au utaratibu wowote mtakaoona unafaa ili mradi miradi hii iweze kuongeza mapato ya Jiji letu” alisema Jafo.
"Sio miradi hii inakamilika ndio mnaanza kutafutana hamjui nini cha kufanya, mnatakiwa muanze kujipanga kuanzia sasa namna gani miradi hii itajiendesha kibiashara na kuleta faida kubwa zaidi, "alisema.
Aidha aliongeza kuwa hili ndio litakua soko la pili la kimataifa baada ya kariakoo na na hili litakua la kisasa na bora zaidi kwa kuwa limejengwa kukidhi mahitaji ya wakazi wa makao makuu ya Nchi na linaendana na hali ya sasa hivyo linahitaji uongozi makini utakaoweza kulisimamia na kuliendasha kwa faida.
Kwa kuongezea Jafo ametoa wito kwa Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Patrobas Katambi na Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma Godwini Kunambi kudumisha ushirikiano katika kusimamia miradi ya umma ili kuleta maendeleo chanya katika jiji la Dodoma kwani ushirikiano ndo silaha kubwa katika kutekeleza uongozi wowote.
Awali ya yote Jafo ametoa pongezi kwa Kampuni ya Mohammed Builders, Kampuni ya hapa nchini ambayo inafanya vizuri katika ujenzi wa miradi mbalimbali waliyopewa kuitekeleza katika Jiji la Dodoma kupitia mradi wa mpango miji mkakati unaotekelezwa kupitia fedha za mkopo toka Benki ya Dunia.
Naye Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Mhe. Patrobas Katambi alisema kuwa yeye na watendaji wake wako imara katika kusimamia sheria,taratibu na kanuni za nchi ili kuongeza chachu ya maendeleo katika jiji la Dodoma.
Mhe. Katambi alisema kuwa yeye na timu watahakikisha wanasimamia miradi ya maendeleo vyema na kukusanya kwa makini mapato ya jiji; Pia watahakikisha mapato hayo yanatumika kuleta maendeleo kwa wana Dodoma na watanzania kwa ujumla kwani Dodoma ndo makao makuu ya Nchi hii.
“Mh.Waziri nikuombe unifikishie salamu zangu kwa Mh.Rais kuwa Dodoma pako salama na wala hakunamigogoro katika uongozi wetu na tunatekeleza majukumu yetu kwa makini na kwa kuzingatia Ilani ya Chama cha Mapinduzi ” Alisema Katambi.
Kwa kuhitimisha Mkurugenzi wa Jiji Godwini Kunambi alisema kuwa Jiji wamejipanga ifikapo 2021 panapo majaaliwa jiji la Dodoma linaweza kujitegemea kwa mapato bila kutegemea ruzuku toka Serikali Kuu.
“Mh.Waziri ili tuweze kufikia malengo ya jiji 2021 kuweza kujiendesha lazima tuwe na kampuni ya jiji itakayoweza kusimamia na kuendesha miradi yote itakayokuwa ikitekelezwa ndani ya jiji letu na nikuhaidi kuwa tutatekeleza vyema maagizo yako.”
Kunambi alimalizia kuwa;" sisi kama Jiji jukumu letu kubwa ni kutoa huduma kwa wananchi hivyo ili miradi hii iweze kufanya biashara tutaanzisha Kampuni kama tulivyoelekezwa, ambayo itakua inajitegemea na itahusika na uendeshaji wa shughuli zote za maeneo ya biashara kama hili soko la kimaita, stendi ya mabasi, stendi ya Malori na maeneo mengine ambayo yatakidhi kutoa huduma za kibiashara "Aliongezea Kunambi.
Katika zaira yake ya siku moja Mhe. Jafo alitembelea na kukagua ujenzi wa stendi ya malori Nala, ujenzi wa kituo afya Mkonze, ujenzi wa Soko la kimataifa Nzuguni pamoja na ujenzi wa stendi ya kisasa.