Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) kimekosoa utaratibu wa kuengua wagombea udiwani 30 wa vyama vya upinzani katika uchaguzi wa marudio.
Juzi, Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) ilitangaza kuwa wagombea wa udiwani 30 kutoka Chama Cha Mapinduzi (CCM) wamepitishwa bila kupingwa baada ya wagombea wa vyama vya upinzani kuenguliwa kwa madai ya kutokidhi vigezo.
Katika taarifa yake iliyotolewa kwa vyombo vya habari jana, Mkurugenzi Mtendaji wa LHRC, Anna Henga, alieleza kuwa kuenguliwa kwa wagombea hao kumewanyima haki ya kushiriki uchaguzi mdogo, huku akidai kuwa hoja zilizotumika kuwaengua hazina mashiko.
"Baadhi ya wagombea hususan wa vyama vya upinzani wameenguliwa katika mchakato wa uteuzi wa wagombea kwa sababu mbalimbali zikiwamo tuhuma za kutokidhi vigezo vya kiufundi, kisheria kwa kutokujua kusoma na kuandika pamoja na vigezo vya kutokuwa raia," Henga alieleza katika taarifa hiyo.
Mkurugenzi huyo alisema Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inasema ni marufuku kwa mtu yeyote kubaguliwa na mtu au mamlaka yoyote inayotekeleza madaraka yake chini ya sheria au utekelezaji wa kazi au shughuli ya mamlaka ya nchi.
“Ikumbukwe nchi yetu ni ya kidemokrasia na inafuata misingi ya mfumo wa nyama vingi tangu mwaka 1992, Sheria ya Vyama vya Siasa imeweka mfumo wa vyama vingi, ni vyema usawa ukazingatiwa pasipo ubaguzi wa aina yoyote ili kuweka mazingira ya uchaguzi kuwa huru na yenye uwazi,” alisema.
Aliongeza kuwa kituo kinaisihi NEC kuzingatia misingi ya demokrasia na kutenda haki katika kusimamia uchaguzi nchini, ikiwa ni pamoja na wananchi na mamlaka za serikali kuheshimu misingi ya kikatiba na kisheria katika kutekeleza majukumu yake.
Henga pia alisema LHRC inapinga vikali kauli ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola ya kuagiza askari kuwalaza mahabusu madereva watakaosababisha ajali kutokana na ubovu wa gari.
"Kauli hii inakiuka miongozo ya kikatiba inayoweka misingi ya dhamana pamoja na dhana ya kutokuwa na hatia mpaka pale itakapothibitika kama ilivyoainishwa katika Ibara ya 13(6)(b) ya Katiba," Henga alisema.
Mkurugenzi huyo alisema kitendo hicho kinaweka mazingira magumu kwa mtuhumiwa kufikia haki ya kupata dhamana kama haki ya kikatiba na kusababisha kuchelewa kwa haki au kukosa kabisa haki ya dhamana kwa kuwa haki iliyocheleweshwa ni haki iliyonyimwa.
Alisema Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai inaweka bayana taratibu za kuchukua dhidi ya watu wanaotuhumiwa kwa makosa mbalimbali na kwamba kwenda kinyume cha utaratibu wa kisheria ni kupuuza utawala wa sheria.
“Kituo hakitosita kumfikisha kiongozi yeyote mahakamani atakayetoa maagizo yanayokiuka misingi ya mikataba ya kimataifa inayolinda haki za binadamu, katiba na sheria za nchi,” alisema.
Henga alisema kituo hicho pia kimeshtushwa na mfululizo wa vitendo na kauli zinazotolewa na viongozi wa serikali zinazokiuka katiba na sheria za nchi.
Alisema kuwa kupitia barua ya Ofisi ya Mkurugenzi wa Mji wa Tunduma mkoani Songwe yenye kumbukumbu namba TTC/01/89/49 kwenda kwa watendaji wa kata wote kuwazuia kutoa barua za kuwawekea dhamana wanaokabiliwa na mashauri ya polisi na mahakamani, inakinzana na haki za binadamu.