MWANDISHI: EDDAZARIA G.MSULWA
ILIPOISHIA
Nikaichukua simu na kuiweka mfukoni mwangu.
“Ila kaka Dany na huo upara huko kichwani mmmmm”
“Una nini?”
“Ahaaa sijazungumza mimi”
Nikakumbatiana nao wote watatu, kisha nikaingia kwenye gari, nikafunga mkanda na kufungua kioo kidogo. Mama akanifwata na kuinama kidogo.
“Hakikisha unarudi na kichwa cha K2 hapa sawa”
Maneno ya mama yakanifanya nimtumbulie macho, akanikazia macho na kunifanya nimjibu bila kupenda kwa kutingisha kichwa.
ENDELEA
Mama akanishika shavu lango na kulifinya kidogo kisha akasimama akiwa na sura iliyo jaa tabasamu. Asma akainama pale alipo kuwa ameinama mama na kunibusu mdomoni mwangu.
“Mwanao nitahakikisha anakua katika mazingira mazuri ya kupendeza”
“Asante mke wangu”
“Kuwa makini lakini”
“Usijali katika hilo”
Asma akanibusu tena. Diana akanipungia mkono, taratibu nikafunga kioo cha gari langu, na taratibu nikaanza kuondoka katika eneo la nyumba hili huku nikiwatizama kupitia kioo cha pembeni jinsi wanavyo nitazama. Ramani iliyopo kwenye tv ndogo ya hili gari, inaaniongoza njia za kupita kwa kutumia kijimshale maalumu cha kunielekezea. Mwendo wa masaa mawili nikawa nimefanikiwa kutoka msituni na kuingia kwenye kijiji kimoja ambacho sikukifahamu kinaitwaje. Ni kijiji kilicho jaa watu wengi pamoja na nyumba za udongo.
Nikaendelea kuifwatisha ramani hiyo hadi nikatokea mji mmoja unao itwa Soni. Sikuhitaji kusimama sehemu yoyote zaidi ya kuendelea na safari yangu ambayo ni ndefu sana bado sijafahamu huko mbele nitakutana na changanoto gani.
Kutokana sio mara yangu ya kwanza kupita kwenye hii barabara ya Soni kuelekea Mombo, nikawa makini sana kwenye kuhakikisha kona zote ninazipita kiusalama, hata mwendo wangu wa gari nikawa nimeupunguza kwa kiasi kikubwa. Nikiwa katikati ya kona, nikakutana na foleni kubwa za magari yaliyo simama, jambo ambalo si la kawaida kwa njia hii kuwa na foleni kubwa kiasi hichi. Ikanibidi na mimi kuweza kusimamisha gari langu huku nikiwa na wasiwasi mkubwa sana. Nikataka kushuka ila roho yangu ikasita kidogo.
Nikiwa nimetulia huku nikisubiria foleni hiyo kwenda mbele, nikaona watoto wawili wakiwa wanatembea kwa miguu wakitokea huko ilipo foleni, taratibu nikafungua kioo cha gari ili niweze kuwauliza kitu.
“Nyie watoto kuna nini huko chini?”
Wakanitazama pasipo kujibu kitu chochote, akilini mwangu nikajiuliza hawaelewi Kiswahili au ndio ukimya.
“Eti watoto wazuri kuna kitu gani kinacho endelea huko chini?”
“Weshu tutonge”
Mmoja alizungumza huku akimvuta mwenzake mkono, kwa haraka haraka nikatambua kwamba neno alilo lizungumza linamsisitizia mwenzake waondoke. Wakaondoka pasipo kunijibu kitu cha aina yoyote, taratibu nikafunga kioo cha gari na kuendelea kusubiria magari yasogee taratibu. Taratibu magari yakaanza kusegea.
Kwa mbali kidogo nikaona askari wa usalama barabarani, wakikagua gari moja baada ya jengine, hapo ndipo wasiwasi ulipo anza kunipanda. Mapigo ya moyo yakanienda mbio sana, kwa maana sikuhitaji kukamatwa mapema kiasi hichi wakati nina jukumu zito mbele yangu. Kutokana gari zimesimama tena nikashuka kwenye gari na kuzunguka kwenye buti la gari, nikalifungua. Begi lenye pesa nikalifungua taratibu pasipo mtu wa gar lililopo nyuma yangu kuweza kuona chochote. Nikachukua kibunda kimoja cha dola za kimarekani, nikalifunga na kurudi ndani ya gari.
Taratibu magari yakaanza kusonga mbele, na mimi nikafika kwenye sehemu ya kukaguliwa. Akanifwata askari wa kike aliye valia sare zake vizuri na kupendeza. Nikafungua kioo cha gar taratibu huku nikiwa nimeandaa noti tano za dola mia. Askari huyo akanitazama kwa sekunde kadhaa kisha akatabasamu.
“Naomba leseni yako”
Nikajifanya ninajipapasa huku kibunda cha noti za kimarekani nikikiweka kwenye siti ya pembeni. Nikamuona askari huyo anavyo tupia jicho lake kwenye kibunda cha pesa hizo.